Guinea: ECOWAS yawawekea vikwazo viongozi wa mapinduzi
Mkutano wa dharura wa Jumuiya ya Kiuchumi ya nchi za Afrika Magharibi, ECOWAS, imechukuwa vikwazo dhidi ya viongozi wa mapinduzi nchini Guinea. Huu ni ujumbe mkali ambao viongozi wa Afrika Magharibi walitaka kutuma kwa utawala wa kijeshi nchini Guinea.
Imechapishwa:
Viongozi wa ECOWAS wameamua kuzuwia mali za kifedha na kuwawekea marufuku ya kusafiri wanachama wa utawala wa kijeshi na ndugu zao, huku wakisisitiza juu ya kuachiliwa kwa rais Alpha Condé.
Mabadiliko ya miezi sita yameombwa
Rais wa jumuiya ya kiuchumi ya mataifa ya Afrika Magharibi ECOWAS, Jean Claude Brou alisema viongozi wakuu wa mataifa ya Afrika Magharibi wamesisitiza pia kwamba hakupaswi kuwepo na haja ya kipindi kirefu cha mpito kwa taifa hilo kurejea kwenye mkondo wa kidemokrasia.
Tayari ECOWAS ilikuwa imeonya kwamba ingewaadhibu watawala wa kijeshi endapo hawangemuachia Condé, ambaye anazuwiliwa katika eneo lisilojulikana tangu alipokamatwa wakati wa mapinduzi ya Septemba 5 mjini Conakry, kwa mujibu wa waziri wa mambo ya nje wa Ghana.
ECOWAS ilikuwa imetuma ujumbe nchini Guinea wiki iliyopita kukutana na kiongozi wa mapinduzi Luteni Kanali Mamady Doumbouya, na ilikuwa inasubiri kuchukuwa uamuzi juu ya namna ya kuushinikiza utawala wa kijeshi kurudi kurudi kwenye utawala wa kikatiba.