Serikali ya Tanzania na Barrick waunda kampuni mpya ya madini
Serikali ya Tanzania na kampuni ya madini ya Barrick zimeunda kampuni moja ya madini.
Imechapishwa:
Kampuni hiyo iliyoundwa itafahamika kwa jina la Twiga Minerals Corporation Limited, kwa mujibu wa waziri wa mambo ya nje wa Tanzania Profesa Palamagamba Kabudi.
Kampuni hiyo itakuwa na makao yake makuu Mwanza, kaskazini magharibi mwa tanzania ambapo serikali ya Tanzania itakuwana umiliki wa hisa asilimia 16 ilihali barrick itakuwa na miliki ya asilimia 84.
Waziri Kabudi amesema hatua hiyo ni mafanikio kwa sekta ya madini nchini Tanzania.
“Nina furaha kubwa mheshimiwa rais alikuwa na hoja. Migodi hii itasimamiwa na Tanzania na itakuwa hapa Tanzania,''amesema Waziri Kabudi ambaye alikuwa kiongozi wa ujumbe wa Tanzania wakati wa muda wote wa mchakato wa majadiliano baina ya serikali na kampuni hiyo yenye makao makuu huko London nchini Uingereza.
Hata hivyo mchakato zaidi wa kisheria unaendelea kupitia ofisi ya mwanasheria mkuu wa serikali ya Tanzania ambapo waziri Kabudi amewaambia wanahabari mjini Dar es Salaam kwamba hatua zote zitakazofuata zitajulishwa kwa umma.
Tangu alipoingia madarakani mwaka 2015 rais Magufuli alianzisha mkakati wa kukabiliana na udanganyifu katika sekta ya madini, mojawapo ya raslimali muhimu inayotegemewa kuingiza mapato ya serikali.