Mugisha Muntu azindua vuguvugu jipya la kisiasa Uganda
Aliyekuwa kiongozi wa chama kikuu cha upinzani nchini Uganda FDC Jenerali Mstaafu Gregory Mugisha Muntu, amezindua vuguvugu jipya la kisiasa, linalofahamika kama The New Formation.
Imechapishwa:
Hatua hii imekuja, baada ya Muntu kusema yeye pamoja na wanachama wengine wa FDC walitofautiana kuhusu mbinu za kupambana na chama tawala NRM, na kumwondoa madarakani rais Yoweri Museveni.
Muntu amewahi kuwa mpinzani wa aliyekuwa mgombea urais Kizza Besigye kuwania tiketi ya kupeperusha bendera ya chama hicho katika Uchaguzi uliopita.
Chama cha FDC kimesema hakiwezi kuwazuia baadhi ya wanachama wake kutofanya maamuzi wanayotaka katika ulingo wa kisiasa nchini humo.
Kuna habari ambazo zimekuwa zikirushwa mitandaoni zikizungumza kwamba Jenerali Mugisha Muntu ameanza kuwasiliana na Mbunge wa upinzani aliyechaguliwa katika eneo la Kyandodo Mashariki mwa Uganda, na mwanamuziki maarufu Robert Kyagulanyi, anayefahamika kwa jina la Bobi Wine.
Robert Kyagulanyi alichaguliwa kuwa mbunge katika uchaguzi mdogo baada ya kusimama kama mgombea huru mwaka uliyopita wilayani Kyadondo mashariki, mwa Uganda.
Robert Kyagulanyi amekua mwiba kwa utawala wa Yoweri Museveni.
Bobi Wine na wenziwe 32 walikamatwa baada ya kudaiwa kushambulia msafara wa Rais wa Yoweri Museveni mjini Arua mwezi uliopita na kuwekwa katika kizuizi cha jeshi.
Mwanzo alipandishwa katika mahakama ya kijeshi kabla ya kuhamishiwa kwenye mahakama ya kiraia na kushtakiwa kwa kosa la uhaini.