Kremlin: Yulia Borisovna Navalnaya 'amepoteza uraia wa Urusi'
Kremlin imetangaza siku ya Jumatatu Machi 18 kwamba Yulia Borisovna Navalnaya, ambaye alichukua mikoba ya marehemu mumewe, mkosoaji kuu wa Kremlin na kiongozi wa upinzani nchini Urusi Alexeï Navalny, amepoteza "mizizi" ya asilia yake na "uraia" wa Urusi, baada ya kuchaguliwa tena kwa Vladimir Putin kwa 87% ya kura.
Imechapishwa: Imehaririwa:
"Yulia Navalnaya huyu mliyemtaja anazidi kuwa mmoja wa watu wanaopoteza mizizi yao, wanaopoteza uhusiano wao na taifa, wanaopoteza uelewa wao wa Nchi yao, hawana tena huruma ya nchi yao," Dmitri Peskov, msemaji wa ofisi ya rais wa Urusi almesema, akijibu swali la mwandishi wa habari.
"Bila shaka niliandika jina 'Navalny"
Wakati wa kampeni za uchaguzi wa rais, Yulia Borisovna Navalnaya alitoa wito kwa raia wa Urusi "kupigia kura mgombea yeyote isipokuwa Putin". Jumapili hii, pia alitangaza kuwa aliandika "Navalny" kwenye kura yake, baada ya kupiga kura katika ubalozi wa Urusi huko Berlin.
"Ni kweli, niliandika jina 'Navalny' kwa sababu haiwezekani (...) kwamba mwezi mmoja kabla ya uchaguzi, mpinzani mkuu wa Putin, ambaye alikuwa kizuizini, anauawa," alisema. Alipoingia ndani ya jengo la ubalozi wa Urusi nchini Ujerumani, wafuasi wake waliimba “Yulia, Yulia, tuko pamoja nawe!”
Yulia Borisovna Navalnaya amejitolea kuendelea na kazi ya mumewe na alitangaza mara kadhaa katika siku za hivi karibuni kwamba Vladimir Putin "alimwua" mumewe, shutma ambayo Kremlin inakanusha vikali.
Alexeï Navalny, mkosoaji mkuu wa Vladimir Putin kwa zaidi ya miaka 10, alifariki mnamo Februari 16 akiwa na umri wa miaka 47 katika koloni la adhabu huko Arctic, ambapo alikuwa akitumikia kifungo cha miaka 19 jela kwa "itikadi kali".