Wenyeji Australia watawala Michezo ya Jumuiya ya Madola, Kenya yashindwa Marathon
Michezo ya Jumuiya ya Madola imekamilika mjini Gold Coast nchini Australia siku ya Jumapili.
Imechapishwa:
Wenyeji wamemaliza wa kwanza kwa kupata medali 198, 80 za dhahabu, 59 za fedha na 59 za shaba.
Uingereza imekuwa ya pili kwa medali 136, huku India ikimaliza tatu bora kwa medali 66.
Afrika Kusini imamaliza katika nafasi ya sita duniani, ikiwa ya kwanza Afrika kwa medali 37, ikifuatwa na Nigeria ambayo imeshikilia nafasi ya tisa kwa medali 24.
Kenya imemaliza ya 14 duniani na ya tatu barani Afrika kwa medali 17, zikiwemo nne za dhahabu huku Uganda ikimaliza katika nafasi ya 15 duniani kwa medali sita, zikiwemo tatu za dhahabu.
Michezo hii imemalizika kwa mbio za Marathon kwa wanaume na wanawake.
Mabingwa wa mbio hizi ndefu, ambao ni wanariadha kutoka Kenya wameshindwa kupata medali huku Michael Shelley kutoka Australia akishinda Marathon kwa upande wa wanaume, akifuatwa na Mganda Munyo Solomon Mutai.
Kwa upande wa wanawake, Mwanariadha kutoka Namibia Helalia Johannes alishinda medali ya dhahabu huku medali ya fedha ikimwendea Lisa Weightman kutoka Australia.
Mbali na riadha, timu ya taifa ya wanaume ya Australia imeshinda dhahabu katika mchezo wa Kikapu huku New Zeland ikishinda dhahabu jatika mchezo wa raga kwa wachezaji saba kila upande.
Michezo ijayo ya Jumuiya ya Madola itafanyika mwaka 2022 jijini Birmingham nchini Uingereza.