Waasi wa Syria watangaza kuuteka mji wa Jarablus
Uturuki na majeshi ya muungano wa kimataifa dhidi ya wanajihadi wamezindua operesheni Jumatano hii Agosti 24 dhidi ya kundi la Islamic State katika mji wa Syria wa Jarablus, kwenye mpaka na Uturuki. Vifaru kadhaa vya Uturuki viliingia katika ardhi ya Syria.
Imechapishwa:
Rais wa Uturuki, Recep Tayyip Erdogan, ametangazakulilenga kundi la IS, lakini pia wanamgambo wa Kikurdi. Serikali ya Damascus imelaani uchokozi dhidi ya uhuru wa taifa lake.
Waasi wa Syria wanaoungwa mkono na Uturuki wametangaza Jumatano hii Agosti 24 kuwa wameuteka mji wa Syria wa Jarablus uliyokuwa ukishikiliwa na kundi la Islamic State, baada ya mashambulizi ya masaa machache yaliyoanzishwa na Uturuki alfajiri kwa lengo la kuwatimua wanajihadi wa kundi la IS. Msemaji wa kundi la waasi amesema kuwa wanajihadi walikuwa wameondoka mji huo kuelekea mji wa Al-Bab, kusini magharibi mwa mji wa Jarablus.
Jeshi la Uturuki, likisaidiwa na majeshi ya muungano wa kimataifa dhidi ya wanajihadi, lilizindua kabla ya alfajiri operesheni inayojulikana kwa jina la "ngao ya mto" kwa lengo la kulitimua kundi la IS katika mji wa Jarablus, mji wa mpakani wa Uturuki. Mapema mchana, waasi 1,500 wa Syria wakisaidiwa na serikali ya Ankara walikuwa tayari kukiteka kijiji cha Keklija, kilomita 5 magharibi mwa mji wa Jarablos.
Uwezo uliyotumiwa na Uturuki ni mkubwa: Vifaru vingi vilivuka mpaka kwa minajili kushambulia ngome za wanajihadi. Kabla ya alfajiri, ndege za kivita aina ya F16 za jeshi la Uturuki zilishambulia ngome zilizoko upande wa pili wa mpaka.