Mwanasiasa wa upinzani Tanzania, Tundu Lissu, kuzindua kitabu chake nchini Kenya.
Mwanasiasa wa Upinzani kutoka nchini Tanzania Tundu Lisu kupitia mwanasheria wake, George Wajackoya, amethibitisha kuwasili nchini Kenya, ambapo siku ya Ijumaa atazindua kitabu chake kinachohusu masuala ya utawala bora katika nchi za Afrika Mashariki.
Imechapishwa:
Katika kitabu chake, Tundu Lissu, amezungumzia mabunge ya nchi za Afrika Mashariki, anayosema yameshikiliwa mateka na Serikali.
Lissu katika maelezo yake amesema nchi za Tanzania na Uganda bado zinashuhudia utawala wa kibabe, miongo kadhaa tangu wakoloni Waingereza waondoke.
Tundu Lissu, amekuwa akiishi uhamishoni nchini Ubelgiji tangu mwezi Novemba mwaka 2020 ambapo alikimbia nchi yake kwa hofu ya usalama baada ya kunusurika jaribio la kuuawa mjini Dodoma wakati akiwa mbunge.
Mwanasiasa huyo ambaye alikuwa mkosoaji mkubwa wa Serikali ya Marehemu John Magufuli, alishirikia uchaguzi wa mwezi Octoba mwaka jana ambapo alishindwa, akisema haukuwa uchaguzi huru na haki na ulitengenezwa kumpendelea rais Magufuli ambaye alifariki mwaka huu.