Jaji Osuji raia wa Nigeria achaguliwa kuwa rais mpya wa Mahakama ya ICC
Chile Eboe-Osuji, amechaguliwa kuwa rais mpya wa Mahakama ya Kimataifa ya uhalifu wa kivita ICC, yenye makao yake jijini Hague nchini Uholanzi.
Imechapishwa: Imehaririwa:
Jaji huyo raia wa Nigeria, ataongoza Mahakama hiyo kwa muda wa miaka mitatu kati ya mwaka 2018-2021 pamoja na manaibu wake Jaji Robert Fremr kutoka Jamhuri ya Czech aliyechaguliwa Makamu wa kwanza wa rais.
Mwingine, aliyechaguliwa ni Makamu wa pili wa urais Jaji Marc Perrin de Brichambaut raia wa Ufaransa.
“Ni heshima iliyojee kuchaguliwa na wenzangu.Ninapoanza majukumu yangu, nategemea kupata uzoefu na ushauri kutoka kwa manaibu wangu,” amesema Osuji.
Osuji ambaye anakumbukwa sana kuongoza kesi dhidi ya rais wa Kenya Uhuru Kenyatta na naibu wake William Ruto, anachukua nafasi ya Jaji Silvia Fernandez de Gurmendi na waliokuwa manaibu wake Joyce Aluoch na Kuniko Ozaki.
Rais huyo mpya wa ICC, akisaidiana na Kiongozi wa Mashtaka Fatou Bensuda kutoka Gambia wana kazi ya kusimamia shughuli za Mahakama hiyo.