Wanachama 100 wa UN watia saini mkataba unaokataza matumizi ya watoto jeshini
Hatimaye nchi mia moja wanachama wa baraza la Umoja wa Mataifa wametia saini mkataba wa kimataifa unaokataza utumikishwaji wa watoto katika majeshi.
Imechapishwa:
Mkataba huo ambao umeelezwa kuchukua muda kutiwa saini ulijadiliwa mara ya mwisho mwaka 2007 katika mkutano uliofanyika jijini Paris ambapo nchi zinazotuhumiwa kuongoza kwa watoto kutumikishwa katika majeshi yao walitakiwa kutia saini.
Akiongea baada ya mkutano wao balozi maalumu wa Ufaransa kwenye kamati ya haki za binadamu Farncois Zimeray amesema kuwa mkataba huo pia umetiwa saini na nchi za Angola, Armenia, Bosnia, Costa Rica na San Marino wakati wa mkutano unaoendelea wa baraza la Umoja wa mataifa jijini New York Marekani.
Hatua hiyo inakuja kufuatia ripoti ya shirika la watoto duniani iliyobainisha kuwa inakadiriwa zaidi ya watoto laki moja wanatumikishwa katika majeshi ya nchi mbalimbali duniani.