Japan: Mbio za kumtafuta mrithi wa Waziri Mkuu Shinzo Abe zaanza
Siku moja baada ya Waziri Mkuu wa Japan Shinzo Abe kutangaza kujiuzulu, mbio za kumtafuta mrithi wake zimeanza leo Jumamosi ambapo majina ya wagombea wa kwanza yameanza kutolewa katika chama chake.
Imechapishwa:
Shinzo Abe, 65, ambaye yuko madarakani tangu mwishoni mwa mwaka 2012, alisema siku ya Ijumaa kwamba anajiandaa kuachia ngazi kutokana na kurudi kwa ugonjwa sugu wa matumbo.
Ugonjwa huu ulikuwa moja ya sababu za kuhitimisha muhula wake wa kwanza kama Waziri Mkuu mnamo mwaka 2007, baada ya kuhudumu mwaka mmoja.
Hata hivyo, Abe alisema ataendelea kusalia madarakani hadi mrithi wake atakapoteuliwa.
Njia za mchakato huu bado hazijaamuliwa. Kulingana na vyombo vya habari vya Japani, mambo kadhaa yanajadiliwa.
Chama cha kisiasa cha Bw Abe cha PLD, kinaweza kuchagua kiongozi mpya kwa kufanya uchaguzi wa ndani wa kawaida, uutakaowajumuisha wabunge wake na wajumbe wote wa chama katika ngazi ya kitaifa.
Lakini kutokana na dharura ya hali hiyo na dharura ya kiafya inayotokana na janga la Corona ambalo linazuia mikusanyiko mikubwa, chama cha PLD kinaweza kuamua kufanya mchakato wa uchaguzi mdogo na wa haraka, ambapo wabunge wake tu na wawakilishi wa raia waliochaguliwa katika majimbo watatakiwa kushiriki.
Utaratibiu wa uchaguzi unatarajiwa kuamuliwa katika wiki ijayo.