China: Raia wawili wa Canada wafunguliwa mashitaka ya kuiba siri za serikali
China imewafungulia mashtaka raia wawili wa Canada kwa madai ya kufanya kazi za kijasusi nchini humo, miezi 18 baada ya kukamatwa na kuzua mvutano wa kidiplomasia kati ya Beijing na Ottawa.
Imechapishwa:
Raia hao wawili wa Canada, mwanadiplomasia wa zamani Michael Kovrig na mfanyibiashara Michael Spavor, walikamatwa muda mfupi baada ya Mkurugenzi wa Kampuni ya Huawei Meng Wanzhou kutiwa mbaroni na kuonekana kama hatua ya China kulipiza kisasi.
Mahakama ya Juu nchini China imethibitisha kuanza kusikiliza kesi dhidi ya wawili hao kwa madai ya kufanya kazi za kijasusi na kuiba siri za serikali.
Hatua hii pia imekuja baada ya Mahakama nchini Canada kuamua kuwa Mkurugenzi huyo wa kampuni ya Huawei atasafirishwa nchini Marekani kufunguliwa mashataka kwa madai kuwa kampuni hiyo ilikiuka masharti ya vikwawo dhidi ya Iran.
Kesi hizi mbili zimeendelea kuhatarisha uhusiano wa kidiplomasia kati ya mataifa hayo mawili na hata kuyumbisha shughuli za kibiashara kati ya mataifa hayo mawili.