Ufilipino: Rodrigo Duterte atawazwa kwa kipindi cha miaka sita
Nchini Ufilipino, Rodrigo Duterte anachukua mamlaka ya uongozi wa nchi Alhamisi hii Juni 30. Mapema mwezi Mei, mwanasheria wa zamani wa miaka 71 alipata ushindi mkubwa katika uchaguzi wa urais, baada ya kampeni iliyowavutia raia wengi wa nchi hiyo.
Imechapishwa:
Wakati wa kampeni yake, Rodrigo Duterte aliahidi hasa kuangamiza maelfu ya wahalifu kutoka miezi ya kwanza baada ya kuchukua hatamu ya uongozi wa nchi. Tangu kuchaguliwa kwake, hajabadilika hata hata kidogo kwa kauli zake, jambo ambalo limekua likiukera Umoja wa Mataifa. Jumatatu wiki hii alikua bado akitetea ahadi yake ya kupambana dhidi ya uhalifu na alishtumu watetezi "wajinga" wa haki za binadamu, akithibitisha kwamba adhabu ya kifoitatumika kwa ajili ya kulipiza kisasi.
Kanisa Katoliki nchini Ufilipino, tayari ililaani, zaidi ya siku kumi zilizopita, tangu kuchaguliwa kwa Rodrigo Dulerte, vifo vya watu wanaoshukiwa kuwa walanguzi wa madawa ya kulevya, labda kwa sababu walipinga kukamatwa kwao. Muda mfupi baada ya ushindi wake, Rodrigo Duterte aliahidi kuwatuza askari polisi ambao watawaua wafanyabiashara wa madawa ya kulevya na kuwahimiza wananchi kuwaua au kuwakamata watuhumiwa wa biashara hiyo haramu.
Rais mpya wa Ufilipino pia alisema kuwa waandishi wa habari "hawatakiwi kuuawa" kama watakuwa wamepewa rushwa. Pia alitangaza kupiga marufuku kuuzwa kwa pombe wakati wa usiku na kuweka amri ya kutotoka nje usiku kwa watoto.
Duterte, hatimaye amewataka waasi wa kikomunisti kuweka silaha chini, wakati ambapo mazungumzo ya amani yanafunguliwa mwezi ujao nchini Norway. Pia amewashangaza wengi kwa kutaja uwezekano wa mazungumzo na kundi la wapiganaji wa Kiislam la Abu Sayyaf, linalojihusisha na utekaji nyara na kuwaua mateka.