Chad: kiongozi wa waasi Timan Erdimi arejea Ndjamena
Kiongozi wa waasi wa UFR, Union of Resistance Forces, amerejea katika mjii mkuuwa wa Ndjamena nchini Chad Alhamisi hii asubuhi. Huyu ni mpwa wa rais wa zamani Idriss Déby Itno, ambaye alikuwa mkuu wa safu ya waasi ambayo ilishuka kwenye mji mkuu mnamo mwaka 2019 na ambayo ilizuiliwa na mabomu 2,000 yaliyorushwa na jeshi la Ufaransa.
Imechapishwa:
Timan Erdimi amerejea nyumbani baada ya miaka 17 akiwa uhamishoni. Kiongozi huyu wa UFR ni miongoni mwa viongozi wa makundi ya waasi waliotia saini kwenye makubaliano ya Doha nchini Qatar.
Timan Erdimi alishuka kwenye ndege iliyomrudisha Ndjamena asubuhi na mapema akiweka kitanga cha mkono wake wa kulia kifuani. Timan Erdimi amepokelewa kwenye uwanja wa ndege na watu ishirini kutoka familia yake licha ya mvua nyingi iliyokuwa ikinyesha.
Pia kulikuwa na wanasiasa kutoka kwa familia yake kama Yaya Dillo Djerou. Timan Erdimi amesema ana furaha kubwa kuona anarejea nyumbani baada ya miaka 17 akiwa uhamishoni, akimuona binti yake, wajukuu zake na jamaa zake, amethibitisha kuwa sasa ni muhimu kushiriki katika ujenzi wa Chad na, amebaini atashiriki katika mazungumzo ya kitaifa yatakayofanyika siku zijazo, Agosti 20 huko Ndjamena. Takriban dakika ishirini baada ya kuwasili, ametoka uwanja wa ndege huku akishangiliwa na jamaa zake, na kusindikizwa na idadi kubwa ya wanajeshi hadi hotelini alikofikia.
Akiwa uhamishoni kwa miaka mingi baada ya kujaribu kumpindua rais wa zamani Idriss Déby Itno, Timan Erdimi alirejea N'Djamena siku ya Alhamisi, siku mbili kabla ya mazungumzo ya kitaifa kati ya upinzani wa kiraia na wenye silaha na utawala wa kijeshi. Kiongozi wa Muungano wa Majeshi ya Upinzani (UFR) atashiriki, kuanzia Jumamosi, katika mazungumzo makubwa ya kitaifa ambayo ndio njia ya mchakato wa uchaguzi "huru na wa kidemokrasia".
Siku ya Jumanne usiku waasi wengine waliokuwa uhamishoni, akiwemo Gassim Cherif, kiongozi wa kundi lililojitenga na CCMSR, kundi jingine muhimu lenye silaha nchini Chad, walirejea nchini.