Somalia: Pande zinazokinzana zatakiwa kutatua tofauti zao kwa maslahi ya taifa
Umoja wa Mataifa, umewataka viongozi wa siasa nchini Somalia, kutekeleza makubaliano yao ya kufanyika kwa uchaguzi wa wabunge ambao sasa umepangwa kufanyika ifikapo Februari 25.
Imechapishwa:
Hatua hii imekuja baada ya mashauriano kati ya Waziri Mkuu Mohamed Hussein Roble na viongozi wa majimbo ambao wamekubaliana kuhusu kalenda hiyo mpya.
Mchakato wa uchaguzi ulipaswa kumalizika mwishoni mwa mwaka uliopita, lakini mvutano kati ya rais na Waziri Mkuu, umeendelea kuchelewasha uchaguzi huo katika taifa hilo la pembe ya Afrika.
Hivi karibuni Rais wa Somalia Rais Mohamed Abdullahi Mohamed Farmajo, alijaribu kumtimua waziri mkuu. Waziri Mkuu Mohamed Hussein Roble alishutumu kile alichokiita "jaribio la mapinduzi dhidi ya serikali" na kuwataka wakuu wa vikosi vya usalama kuchukua maagizo yao kutoka kwake na sio kutoka kwa rais.
Washirika wa Somalia, sawa na baadhi ya nchi 20 na mashirika ya kimataifa, yalielezea wasiwasi wao katika taarifa kwa vyombo vya habari kuhusu mvutano huo.