Takriban watu 14 wafariki katika ajali ya barabarani huko Sinai nchini Misri
Takriban watu 14 wamefariki dunia na wengine 17 kujeruhiwa alfajiri siku ya Jumamosi katika ajali ya barabarani iliyohusisha basi na basi dogo katika rasi ya Sinai Kusini mwa Misri, maafisa wa usalama wamesema.
Imechapishwa:
Ukungu na mwendokasi mwingi wa madereva hao wawili ndio chanzo cha ajali hii iliyotokea karibu na El-Tor, mji mkuu wa mkoa wa Sinai Kusini, kilomita 400 kusini-mashariki mwa Cairo, - vyanzo hivyo vimebaini.
Basi hilo lilikuwa likitoka Cairo na lilikuwa likielekea mji wa mapumziko wa Sharm el-Sheikh kwenye Bahari Nyekundu lilipogongana na basi dogo.
Majeruhi wote wamepelekwa hadi hospitali katika mji wa El-Tor.
Ajali nyingi hufanyika nchini Misri ambapo barabara hazifanyiwi ukarabati na sheria za barabarani hazitekelezwi hata kidogo.
Kulingana na takwimu rasmi, watu 7,000 walifariki dunia katika ajali za barabarani nchini Misri mnamo mwaka 2020.