Chad: Kiongozi wa waasi Timan Erdimi aweka masharti kwa kushiriki katika mazungumzo
Serikali ya Chad ilizindua rasmi mashauriano ya kisiasa kwa makundi ya waasi Oktoba 18. Lengo ni kuyafanya yashiriki katika mazungumzo ya kitaifa yaliopangwa kufanyika mwezi Novemba, ambayo yanakusudiwa kuwa jumuishi. Timan Erdimi, mkuu wa Muungano wa makundi ya waasi ya UFR ameweka masharti yake kwa kushiriki katika mashauriano hayo.
Imechapishwa:
Kamati Maalum ya Kiufundi, ambayo inaongozwa na rais wa zamani Goukouni Weddeye, ilifanya safari hadi Doha, Qatar, ambako ilikutana na Timan Erdimi. Mkutano huo ulichukua dakika 45, kulingana na Timan Erdimi, akiwa uhamishoni kwa zaidi ya miaka kumi.
Ili kuongoza majadiliano hayo, Kamati Maalum ya kiufundi iliomba msaada kwa Aboubakar Assidick Choroma, balozi wa zamani wa Chad nchini Qatar, lakini pia kwa Jenerali Mahamat Saleh Kaya, mwezeshaji mkuu, kwani mkuu huyu wa zamani wa majeshi katika utawala wa Idriss Déby Itno alikuwa mume wa mmoja wa madada wa Timan Erdimi.
Ombi la msamaha wa jumla au marejesho ya mali
Akiwa hajakatishwa tamaa wala kuridhika na mijadala hiyo, kiongozi wa UFR anaeleza kwamba haoni umuhimu wowote kwenye mazungumzo ya Ndjamena "ambapo hakuna jipya litakalotoka".
Badala yake, UFR inataka mashauriano kati ya makundi ya kisiasa na kijeshi na mamlaka, na kuweka masharti ikiwa ni pamoja na msamaha wa jumla, kurejeshwa kwa mali iliyotwaliwa na kuachiliwa kwa wafungwa wa kisiasa, hali sawa na zile za makundi mengine ya kisiasa na kijeshi yaliyokutana huko Paris.
Masharti ambayo hayawezekani, kulingana na kamati, ambayo itayawasilisha kwa mamlaka huko Ndjamena, mara tu mashauriano yote yatakapomalizika.