Kifo cha Bouteflika: Algeria yatangaza siku 3 za maombolezo ya kitaifa
Rais wa Algeria ametangaza siku tatu za maombolezo ya kitaifa kuanzia leo Jumamosi Septemba 18, 2021, kufuatia kifo cha rais wa zamani wa taifa hilo, Abdelaziz Bouteflika.
Imechapishwa:
Ofisi ya rais huyo wa sasa imesema katika maombolezo hayo ya siku 3 bendera zitapepea kwa nusu mlingoti.
Habari ya kifo cha Abdelaziz Bouteflika ilitangazwa na runinga ya taifa ya Algeria, ikinukuu taarifa kutoka ofisi ya rais wa Jamhuri: "Kifo cha rais wa zamani Abdelaziz Bouteflika" iliandikwa kwenye bango jekundu lililokuwa likipitishwa mara kwa mara kwenye runinga ya taifa Ijumaa jioni.
Tangu aachie ngazi baada ya shinikizo kutoka kwa jeshi na maandamano ya kiraia, rais wa zamani wa Algeria alikuwa akiishi katika nyumba yake huko Zeralda, magharibi mwa Algiers. Televisheni za serikali zilitangaza tu kifo cha rais Abdelaziz Bouteflika, bila hata hivyo kukatiza programu zao ili kutoa matangazo maalum kufuatia tukio hilo.
Abdelaziz Bouteflika, ambaye utawala wake wa miaka 20, unatajwa kugubikwa na rushwa na aliondolewa madarakani kwa maandamano makubwa baada ya kutaka kugombea madaraka kwa muhula mpya.