Uchaguzi wa wabunge na kura ya maoni vyasogezwa mbele Guinea
Uchaguzi wa wabunge na kura ya maoni ya katiba havitafanyika Machi 15 nchini Guinea kama ilivyotangazwa na Rais wa nchi hiyo Alpha Condé mwishoni mwa mwezi wa Februari.
Imechapishwa:
Kwa mujibu wa mwenyekiti wa Tume ya uchaguzi nchini Guinea, CENI, hakuna tarehe ambayo imepangwa.
CENI inasubiri ripoti ya ukaguzi itakayotolewa na wataalam wa Jumuiya ya kiuchumi ya nchi za Afrika Magharibi, ECOWAS, kuhusu daftari la kudumu la wapiga kura ili kupanga tarehe mpya.
Uchaguzi wa wabunge na kura ya maoni ya katiba ambayo ilipangwa kufanyika Desemba 28, 2019, kisha ikaahirishwa tena, haitafanyika Jumapili hii, Machi 15, amethibitisha afisa mwandamizi wa CENI, Tume Huru ya Taifa ya Uchaguzi.
Mwishoni mwa mwezi wa Februari, Rais Alpha Condé alitangaza kusogeza mbele wiki mbili uchaguzi huo chini ya shinikizo kutoka kwa upinzani na jamii ya kimataifa, ambao walionyesha wasiwasi wao kuhusu daftari la kudumu la wapiga kura.