Pata taarifa kuu
DRC-SIASA

Serikali ya umoja yaundwa DRC

Hatimaye serikali ya umoja imeundwa nchini Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo, miezi saba baada ya Felix Tshisekedi kutawazwa kama rais wa DRC, amesema Waziri Mkuu Sylvestre Ilunga.

Rais wa DRC Felix Tshisekedi akimpokea Waziri wake mpya Sylvestre Ilunga Ilunkamba Mei 20, 2019, Kinshasa.
Rais wa DRC Felix Tshisekedi akimpokea Waziri wake mpya Sylvestre Ilunga Ilunkamba Mei 20, 2019, Kinshasa. @ Présidence de la République démocratique du Congo
Matangazo ya kibiashara

"Kwa sasa serikali imeundwa. Rais wa Jamhuri, mkuu wa nchi, hatimaye amesaini agizo rasmi. Kwa hivyo sasa, serikali imeundwa, hivi karibuni tutaanza majukumu yetu, "Waziri Mkuu wa DRC, Sylvestre Ilunga, ametangaza katika mkutano na waandishi wa habari, ambaye mwenyewe aliteuliwa Mei 20, 2019.

Kwa mujibu wa vyanzo kadhaa mjini Kinshasa, kuna sura mpya katika baraza hilo jipya la mawaziri ambazo hazijawahi kuwepo katika serikali.

Chama cha rais huyo wa zamani sasa kimepata wizara 43, na kile cha rais Félix Tshisekedi kimejinyakulia wizara 23.

Kama walivyokubaliana, muungano wa CACH wa Rais Tshisekedi umechukuwa Wizara ya Mambo ya Ndani, ambayo imekabidhiwa Gilbert Kankonde Malamba, mshirika wa karibu wa rais wa sasa, ambaye hadi sasa amekuwa katibu wa kitaifa anayesimamia uhusiano wa nje katika chama chake cha UDPS. Muungano huo pia umechukuwa Wizara ya Mambo ya Nje, ambayo imekabidhiwa mwanamke, Marie Tumba Nzeza, ambaye hana umaarufu sana katika siasa.

Muungano wa FCC wa Joseph Kabila umechukuwa wizara ya sheria, ambapo Celestin Tunda Ya Kasende ameteuliwa kama Waziri wa Sheria, na pia Wizara ya Ulinzi ambayo inashikiliwa na Aimé Ngoy Mukena.

Asilimia 17 ya wanawake wameteuliwa katika serikali hiyo mpya.

Awali ripoti kutoka Kinshasa zilisema kuwa, rais Tshisekedi alitaka baraza hilo kupunguzwa kwa nafasi mbili.

Mwishoni mwa wiki hii iliyopita, Waziri Mkuu Ilunga alisema kuwa, zoezi hilo linachukua muda mrefu kwa sababu maeneo yote ya DRC yanastahili kuwakilishwa katika baraza hilo ambalo litaundwa na wanasiasa kutoka upande wa rais Tshisekedi na rais wa zamani Joseph Kabila.

Katika siku zilizopita, kumekuwa na maandamano jijini Kinshasa kutoka kwa wananchi wakihoji ni kwanini imechukua muda mrefu kutangaza majina ya Mawaziri wapya.

Kazi kubwa la serikali mpya inayosubiriwa kwa hamu, kwanza ni kuimarisha usalama Mashariki mwa DRC , kupambana na ugonjwa wa Ebola na kuimarisha maisha ya raia wa nchi hiyo wanaoendelea kuishi kwa umasikini mkubwa licha ya nchi hiyo kuwa na rasilimali nyingi.

Kusambaza :
Ukurasa haipatikani

Maudhui unayojaribu kuyatafuta hayapatikani kwa sasa au yamekwishaondolewa.