Marekani na EU zaitaka DRC kuacha matumizi ya nguvu kubwa kwa raia
Marekani na Umoja wa Ulaya zimevitaka vikosi vya ulinzi nchini Jamhuri ya kidemokrasia ya Congo, kuacha kutumia nguvu kubwa dhidi ya raia baada ya askari kuwafyatulia risasi wakimbizi wa Burundi juma lililopita na kusababisha vifo zaidi ya 30.
Imechapishwa:
Msemaji wa wizara ya mambo ya kigeni Heather Nauertamesema katika taarifa kuwa serikali ya Marekani imeguswa na vurugu na vifo vya watu zaidi ya 30 wa Burundi na askari wa Kongo huko Kamanyola, mashariki mwa Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo na kuitaka serikali ya DRC kuacha kutumia nguvu kubwa.
Kulingana na MONUSCO, ujumbe wa kulinda amani wa Umoja wa Mataifa nchini DRC, takribani wakimbizi 36 huko Kamanyola, katika jimbo la mashariki ya Kusini mwa Kivu, waliuawa katika vurugu siku ya Ijumaa sambamba na Askari mmoja wa Kongo.
Msemaji wa Serikali Lambert Mende amedai kuwa wengi wa waliouawa walikuwa wanachama wa kundi linalomiliki silaha.
Kwa mujibu wa afisa wa wizara ya mambo ya ndani Josue Boji, mapigano yalianza baada ya kikundi cha wakimbizi kuvamia jela inayoendeshwa na taasisi ya intelijensia ya ndani ya nchi ili kutaka kuachiwa kwa wenzao wanne ambao walikamatwa wakitakiwa kurejeshwa kwao.