Niger yajiandaa kuwatuma wanajeshi wake Nigeria
Wabunge wa Niger wamepitisha Jumatatu jioni wiki hii azimio la kutumwa kwa kikosi cha wanajeshi 750 nchini Nigeria ili kulitokomeza kundi la Boko Haram.
Imechapishwa:
Kura hii ilipigwa na Wabunge wote wakiwemo Wabunge wa upinzani. Azimio hili litapelekea wanajeshi wa Niger kujiunga na majeshi ya Cameroon, Chad na Nigeria, ambazo zimeanzisha vita dhidi ya Boko Haram.
Hayo yakijiri kundi la Boko Haram liliendesha Jumatatu wiki hii shambulio katika mji wa Diffa nchini Niger. Kwa mujibu wa vyanzo vya hospitali na mashahidi, shambulio hilo liliendeshwa na mtu aliejitoa muhanga.
Watu 5 wameuawa katika shambulio hilo na wengine 16 wamejeruhiwa wakiwemo 5 ambao wamejeruhiwa vikali.
Wakati huohuo serikali ya Cameroon imeanzisha uchunguzi ili kujua iwapo raia wake waliotekwa nyara na Boko Haram Jumapili Februari 8 wote waliachiliwa huru. Raia wa Cameroon ambao walikua wakisafiri kutoka Koza wakielekea Mora kwenye mpaka wa Nigeria walitekwa nyara na Boko Haram. Kwa mujibu wa mashahidi walionukuliwa na shirika la habari la Ufaransa la AFP, watu 12 miongoni mwa raia hao wa Cameroon waliuawa. Cameroon haijathibitisha.
Nigeria imethibitisha kwamba ngome za Boko Haram katika ardhi yake zitakua zimevunjwa ndani ya majuma sita
Rais wa Niger Mahamdou Issoufou ameapa kulitokomeza kundi la Boko haram.
Wakati ambapo operseheni ya kikanda dhidi ya Boko Haram ikiandaliwa, kiongozi wa Boko Haram, ameelezea msimamo wake katika mkanda wa video uliyorushwa Jumatatu wiki hii. Katika mkanda huo unaodumu dakika 28, Abubakar Shekau amekashifu zoezi hilo la kutumwa kwa wanajeshi kutoka mataifa hayo matatu.
“ Muungano wenu hautazaa matunda yoyote. Kwa hiyo mkusanye silaha zenu kwa kuweza kukabiliana na si. Tunakutakieni mafanikio mema, karibuni”, amesema Shekau
Katika hotuba hii yenye uchokozi, kwa lugha ya Kiarabu na baadae kwa lugha ya Kihausa, kiongozi wa Boko Haram amesema kwa kauli ya dharau: " Mnatuma wanajeshi 7000? 7000 tu, kwa Mwenyezi Mungu ni idadi ndogo mno ! Tutawakama mmoja mmoja."