Niger: Boko Haram yashambulia miji ya Bosso na Diffa
Kundi la Boko haram limeendesha mapema Ijumaa asubuhi mashambulizi katika miji ya Bosso na Diffa nchini Niger kwenye mpaka na Nigeria, katika eneo la Ziwa Chad.
Imechapishwa: Imehaririwa:
Hili ni shambulio la kwanza la aina yake linaloendeshwa na kundi lenye silaha nchini Niger. Majeshi ya Chad na Nigeria yameingilia kati haraka na kudhibiti eneo hilo. Mji wa Diffa umeshuhudia mvua ya mabomu.
Habari bado ni ya kutatanisha, lakini kilicho kweli ni kwamba Ijumaa asubuhi wiki hii wapiganaji wa tawi la kundi la Boko Haram lenye makao yake Malam Fatori, upande wa Nigeria, walipenya bila wasiwasi na kuingia katika mji wa Bosso katika pwani ya Nigeria.
Mashahidi wanasema walisikia milio ya risasi na milipuko ya mabomu karibu sana katika vitongoji vya mji huo.
Vyanzo vya kijeshi eneo hilo vinathibitisha kwamba kulikuwa na mapigano, lakini saa za hivi karibuni jeshi la Chad na vikosi vya Nigeria wamedhibiti eneo kulikotokea. mashambulizi. Mwanajeshi wa Chad ameithibitishia RFI kwamba wanaendelea na operesheni ya kuwasaka wapiganaji hao wa Boko haram upande wa pili wa mto.
Wiki hii, serikali ya Niger ililiomba Bunge la nchi hiyo kutoa ruhusa kwa ajili ya kuingilia kijeshi dhidi ya Boko Haram. Bunge limepanga kukutana Jumatatu asubuhi februari 9, lakini mashambulizi ya Boko Haram yameendelea kushangaza wengi.