Erdogan atishia kuishambulia serikali ya Syria
Katika mazungumzo ya simu leo Jumatano, rais wa Urusi Vladimir Putin na Rais wa Uturuki Recep Tayyip Erdogan wamesema wanapenda kuona "utekelezaji kamili" wa makubaliano ya kupunguza uhasama kati ya Urusi, Uturuki na Syria, hasa katika Mkoa wa Idleb.
Imechapishwa:
Serikali ya Damascus imekuwa ikiendesha mashambulizi mabaya katika Mkoa wa Idlib.
Katika siku za hivi karibuni, vikosi vya Uturuki na Syria vimekuwa vikipambana katika mkoa wa Idleb. Licha ya uhusiano wa kidiplomasia na mazungumzo kati ya Urusi na Uturuki, Rais Erdogan ametoa hotuba ya kujiamni mbele ya kundi la wabunge, akitishia kushambulia vikosi vya serikali ya Syria 'popote pale' kama kutatokea shambulio jipya dhidi yao.
Wanajeshi wanane wa Uturuki waliuawa katika shambulio la vikosi vya Syria huko Idleb.
Wiki moja iliyopita, Recep Tayyip Erdogan alimpa Bashar al-Assad hadi mwisho wa mwezi ili kuwaondoa askari wake katika maeneo yaliyodhibitiwa katika wiki za hivi karibuni.
Katika maeneo haya, jeshi la Uturuki linashikilia ngome 12 za jeshi, chini ya makubaliano ya Urusi na Uturuki yaliyosainiwa katika mji Sochi mwaka 2018.
Erdogan amesema Uturuki imedhamiria kuvirejesha nyuma vikosi vya serikali ya Syria kutoka vituo vyake vya kijeshi kwenye jimbo la Idlib ifikapo mwishoni mwa mwezi Februari.
Machafuko yameongezeka kwenye jimbo la Idlib baada ya vikosi vya serikali ya Syria vinavyoungwa mkono na Urusi kupata mafanikio katika kampeni yake ya kuwatokomeza waasi kwenye vita vya miaka tisa vya nchi hiyo.