Wanajeshi wa Israeli wameripotiwa kutekeleza mashambulio katika mji wa Rafah
Israeli imeripotiwa kutekeleza mashambulio katika mji wa Rafah wenye idadi kubwa ya raia wa Palestina, eneo ambalo tayari imeanza kuendesha oparesheni zake za ardhini.
Imechapishwa:
Hatua hii ya Israeli inakuja wakati huu mazungumzo ya kumaliza mapigano ya miezi saba sasa kati yake na Hamas yakiwa yanaendelea jijini Cairo.
Licha ya pingamizi kutoka kwa jamii ya kimataifa dhidi ya oparesheni hiyo, Israeli ilipeleka magari yake ya kivita katika mji wa Rafah siku ya Jumanne ya wiki hii ambapo ilitangaza kudhibiti mpaka muhimu wa kuingia katika ukanda wa Gaza.
White House ilikashifu hatua hii ya Israeli ya kuhitilafiana na mpango wa ukipelekaji wa misaada ya kibinadamu katika ukanda Gaza, Marekani ikitangaza kusitisha usafirishaji wa mabomu nchini Israeli baada ya tishio la oparesheni za kijeshi katika mji wa Rafah kutoka kwa mshirika wake Israeli.
Saa chache baadae, mamlaka nchini Israeli ilitangaza kufungua mpaka mwengine wa Kerem Shalom unaoingia katika ukanda wa Gaza.
Soma piaIsraeli imefungua tena mpaka wa Kerem Shalom kuruhusu misaada kuingia Gaza
Licha ya tangazo la Israeli la kufungua mpaka huo, shirika la Umoja wa Mataifa kuhusu wakimbizi wa Palestina UNRWA, limesema bado mpaka huo umefungwa.
Mamlaka nchini Israeli ilitangaza kufunga mpaka huo baada ya wapiganaji wa Hamas kurusha kombora siku ya Jumapili na kusababisha vifo vya wanajeshi wanne wa Israeli.
Mapigano yalianza katika ukanda wa Gaza tarehe saba ya mwezi Aprili baada ya wapiganaji wa Hamas kutekeleza shambulio katika ardhi ya Israeli ambapo watu zaidi ya elfu moja waliuawa wengi wao wakiwa ni watoto kwa mujibu wa takwimu rasimi.
Kutokana na shambulio hilo, Israeli iliapa kulipiza kisasi kwa kuwatokomeza Hamas, karibia watu 34,789 wakiwemo watoto na wanawake katika ukanda wa Gaza wakiripotiwa kuuawa katika oparesheni zake dhidi ya Hamas.