Tetemeko la Ardhi: Umoja wa Mataifa waomba karibu dola milioni 400 kwa Syria
Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa amezindua ombi la dharura la michango ya karibu dola milioni 400 kusaidia watu walioathiriwa na tetemeko la ardhi nchini Syria kwa kipindi cha miezi mitatu.
Imechapishwa:
"Leo, ninatangaza kwamba Umoja wa Mataifa unazindua ombi la kibinadamu la dola milioni 397 kwa watu walioathiriwa na tetemeko la ardhi lililoathiri Syria. Hii itachukua muda wa miezi mitatu,” Antonio Guterres amewaambia waandishi wa habari, akiongeza kuwa ombi kama hilo la michango kwa Uturuki liko katika maandalizi.
Hata hivyo Umoja wa Mataifa umesema zaidi ya watoto milioni 7 wameathirika kwa tetemeko la ardhi nchini Uturuki na Syria, yaliyotokea wiki iliyopita.
James Elder, msemaji wa shirika la Umoja wa Mataifa la kuwahudumia watoto, UNICEF, amesema nchini Uturuki pekee idadi jumla ya watoto walioathirika katika mikoa 10 iliyokumbwa na matetemeko hayo mawili ya ardhi ilifikia milioni 4.6. huku Syria ikiwa na watoto milioni 2.5 walioathirika na hali hiyo.
Ameyasema hayo wakati timu ya uokozi ikijianda kukamilisha operesheni zake za kuwatafuta manusura wa janga hilo lililosababisha vifo vya watu zaidi ya elfu35,000 katika mataifa yote mawili.