Hollande azuru Ujerumani kabla ya kukabidhi madaraka kwa Macron
Rais wa Ufaransa anayemaliza muda wake Francois Hollande amefanya ziara yake ya mwisho nchini Ujerumani ambako amekutana na kansela Angela Merkel, ikiwa ni siku chache kabla ya kukabidhi madaraka kwa rais mteule Emmanuel Macron.
Imechapishwa:
Siku ya Jumatatu kabla ya kuelekea Ujerumani, rais Hollande alikuwa pamoja na Macron wakati wa sherehe za maadhimisho ya kumbukumbu ya vita vya pili vya dunia, ambapo alimpongeza kwa ushindi wake na kueleza historia iliyopo ya kukabidhiana madaraka kwa amani.
Katika hatua nyingine viongozi mbalimbali kutoka barani Afrika wameendelea kutuma salaam za pongezi kwa Macron, ambapo rais wa umoja wa Afrika rais wa Guinea Alpha Conde, amesema ana imani kiongozi huyo ana dira nzuri na bara la Afrika na kwamba ushindi wake ni historia mpya kwa taifa hilo na bara la Afrika.
Akiwa nchini Ujerumani Kansela wa Ujerumani Angela Merkel amesema amekuwa mwenye furaha mara zote anapofanya kazi na Hollande na kwamba hivi karibuni atakutana na rais mteule Emmanuel Macron.