Ufaransa kutuma manowari dhidi ya IS
Kufuatia kikao cha baraza la ulinzi, Alhamisi wiki hii, Ikulu ya Elysée imetangaza kuwa Ufaransa itapeleka manowari yake kubwa zaidi ya kivita iitwayo Charles-de-Gaulle nchini Syria na Iraq kushiriki katika operesheni ya kijeshi dhidi ya kundi la Islamic State.
Imechapishwa: Imehaririwa:
Rais wa Ufaransa François Hollande amesema uamuzi huo ni mwafaka na utasaidia Ufaransa kusaidiana vyema na washirika wake.
Serikali ya Ufaransa imesema mashambulio dhidi ya IS ni hatua ya kujikinga, baada ya wanamgambo wa IS kuua watu 17 katika mashambulio mawili mjini Paris mapema mwaka huu.
Kutumiwa kwa meli hiyo ya kivita kutasaidia kupunguza muda unaotumiwa na ndege za kivita kutekeleza mashambulio kutoka angani.
Septemba mwaka huu, Ufaransa ilianza kutekeleza mashambulio ya kijeshi ya angani dhidi ya kundi la wanajihadi la Islamic State.
Manowari hiyo, awali ilitumwa katika Ukanda huo kukabiliana na wapiganaji hao wa Kiislamu.
Manowari hiyo ina uwezo wa kubeba zaidi ya ndege 40 kwa siku na kufanikisha safari 100 za ndege kila siku.
Ufaransa imekuwa ikishambulia IS chini ya muungano unaoongozwa na Marekani tangu Septemba 2014.
Meli hiyo, ndio pekee ya aina yake kumilikiwa na Ufaransa, ilitumiwa kama kituo cha kutua na kupaa kwa ndege za kijeshi za Ufaransa eneo la Ghuba kuanzia mwezi Februari hadi mwezi Aprili.
Ufaransa kwa sasa inatumia ndege sitandogo aina ya Mirage ambazo zinahudumu kutoka Jordan na ndege sita aina ya Rafale ambazo hushambulia IS kutoka Muungano wa Milki za Kiarabu.