Pata taarifa kuu
AFCON 2027

Afrika Mashariki yaanza kujiandaa kuelekea AFCON 2027

Kenya – Mwezi Septemba, Shirikisho la Soka barani Afrika CAF lilitangaza Kenya, Uganda na Tanzania kama waandalizi rasmi wa toleo la 36 la mashindano ya taifa bingwa barani Afrika.

WAZIRI WA MICHEZO NCHINI KENYA NAMWAMBA ABABU
WAZIRI WA MICHEZO NCHINI KENYA NAMWAMBA ABABU © rfi Kiswahili
Matangazo ya kibiashara

Waziri wa michezo nchini Kenya, Ababu Namwamba ametoa hakikisho kuwa Kenya iko tayari zaidi kuandaa mashindano ya kombe la mataifa ya Afrika ya mwaka 2027. 

Waziri Namwamba alikua akizungumza katika kikao cha pamoja cha Afrika Mashariki mjini Diani nchini Kenya, kikao ambacho kilihudhuriwa na wajumbe wa serikali za mataifa hayao matatu na marais wa shirikisho.  

Ababu alieleza kuwa mipango ya ujenzi wa uwanja mpya wa Talanta ambao utachukua muda wa miaka miwili kukamilisha ujenzi.  

“Nilikutana na waziri wa ulinzi pamoja na viongozi wa idara hiyo hivi karibuni ili kujadili mikakati ya ujenzi na ninawahakikishia niliridhika na mipango sababu wao ndio tuliwapa jukumu la ujenzi huo,” alisisitiza Ababu Namwamba ambaye pia alitaja kuwa shughuli ya kuweka jiwe la msingi katika ujenzi wa uwanja huo utafanyika mwezi Desemba mwaka 2023.  

Uganda na Tanzania pia zilifafanua mabadiliko na hali ya viwanja ambayo mataifa yao yanafanyia kazi.  

Rais wa soka nchini Tanzania, Wallace Karia amesema Tanzania tayari itakuwa na viwanja viwili kuandaa mechi zozote kufikia January 24 mwaka ujao - uwanja wa Benjamin Mkapa na uwanja wa Amaan kwenye kisiwa cha Zanzibar ambao utafunguliwa Disemba tarehe 31.  

“Serikali ya Tanzania imetoa ruhusa ya viwanja viwili vyenye idadi ya mashabiki elfu 30, mjini Dodoma na Arusha kujengwa. Pia ujenzi wa barabara za kutoka uwanja wa ndege hadi uwanjani Mkapa umeanza jijini Dar es Salaam,” alisisitiza rais Wallace Karia. 

Zanzibar ambayo ina visiwa viwili, Ugunja na Pemba, uwanja wa Gombani uliopo kwenye kisiwa cha Pemba una kila kitu isipokuwa tu nyasi za kisasa.  

Wawakilishi wa serikali za Kenya, Uganda na Tanzania baada ya kujadiliana kuhusu mipango ya AFCON 2027
Wawakilishi wa serikali za Kenya, Uganda na Tanzania baada ya kujadiliana kuhusu mipango ya AFCON 2027 © rfi Kiswahili

Waziri wa michezo nchini Zanzibar, Tabia Maulid Mwita amesema, “walipokea ushauri wa CAF kuboresha uwanja wa Amaan wakati wajumbe walizuru kufanya ukaguzi na kukuta ukarabati wa uwanja ukiendelea.” Uwanja huo awali ulikua na idadi ya mashabiki elfu kumi na mbili ila sasa umefika watu elfu 15 na kufikia mwaka 2027 idadi ya uwanja itakuwa imefika elfu ishirini.” 

Rais Karia alihakikisha kuwa halmashauri ya manispaa ya Kinondoni ipo kwenye hatua ya mwisho kumaliza ujenzi wa uwanja wao ambao utatumika kama uwanja wa mazoezi. Uwanja wa Azam ambao pia utatumika kama uwanja wa mazoezi utafanyiwa ukarabati hivi karibuni.  

“Ujenzi wa uwanja mpya wa Arusha utaanza rasmi tarehe 24 Januari na ni uwanja wenye idadi ya mashibiki elfu 30. Pia tuna mpango wa kujenga uwanja mwingine mjini Dodoma utakaoitwa Jamhuri,” alielezea Wallace Karia.  

 

Nchini Uganda, mjumbe wa kamati ya shirikisho la soka Rodgers Byamukama ameeleza kuwa nyasi za kisasa na viti vipya vimeanza kuwekwa katika uwanja wa Namboole katika harakati za kumalizia ukarabati wa uwanja huo.  

“Tuna imani kuwa timu ya taifa ya Uganda Cranes itacheza mechi zake za kufuzu Kombe la Dunia la 2026 nchini Uganda baada ya mrefu bila kucheza katika viwanja vya nyumbani,” alisisitiza Rodgers Byamukama.  

Uganda pia ina nia ya kujenga uwanja mpya wa jijini Hoima pamoja na ni kufanya ukarabati wa uwanja wa Nakivubo na Denver Goodwin mjini Entebe.  

Kusambaza :
Ukurasa haipatikani

Maudhui unayojaribu kuyatafuta hayapatikani kwa sasa au yamekwishaondolewa.