Nigeria: Shirikisho la soka linataka kumuongezea mkataba kocha Peseiro
Nairobi – Shirikisho la mpira nchini Nigeria (NFF) limeanzisha mazungumzo na Jose Peseiro kuhusiana na mipango ya kusaini mkataba mpya kama kocha wa timu ya taifa.
Imechapishwa:
Kwa mujibu wa rais wa NFF Ibrahim Gusau, mkataba wa kocha huyo ulimamika mwezi Julai na kwa sasa wanafanya majadiliano naye pamoja na mawakili wake.
Peseiro alikuwa anatumikia mkataba wa mwaka mmoja na kwa mujibu wa Gusau mazungumzo yalifanyika kwa sababu ya kucheleweshwa kwa kombe la mataifa ya Afrika la 2023, ambalo kandarasi hiyo ilizingatia.
Mashindano hayo yatafanyika Januari na Februari. Peseiro ameiongoza Nigeria kufuzu huku ikiwa na mechi moja tu.
Vyanzo vya habari vilisema NFF inataka Peseiro akubali kupunguziwa mshahara wake wa kila mwezi wa $70,000 katika kandarasi mpya ambayo itadumu angalau hadi mwisho wa mashindano nchini Ivory Coast.
“Tunatumai kuhitimisha hivi karibuni na uamuzi utatolewa kulingana na mapendekezo ya kamati ya kiufundi,” alisema Gusau.
Super Eagles wakamilisha kampeni yao ya kufuzu Septemba 10 wakiwa nyumbani dhidi ya Sao Tome na Principe.
Gusau alisema mkataba wa kocha Randy Waldrum wa timu ya wanawake ya nchi hiyo pia umemalizika baada ya kuiwezesha kutinga hatua ya 16 bora ya kombe la dunia la wanawake nchini Australia na New Zealand.
Alisema uamuzi kuhusu Waldrum pia utalazimika kuchukuliwa hivi karibuni, kwani timu hiyo itaanza kampeni ya kufuzu kwa michezo ya olimpiki ya Paris ya 2024 mwezi ujao.