Asamoah Gyan wa Ghana ametangaza kustaafu soka
NAIROBI – Nyota wa soka wa Ghana Asamoah Gyan ametangaza rasmi kustaafu soka. "Ni wakati wa kutundika jezi na buti kwa utukufu ninapostaafu rasmi kutoka kwa mpira wa miguu.'' Gyan alisema katika taarifa kwenye ukurasa wake wa Twitter.
Imechapishwa:
Mshambuliaji huyo alifunga mabao 51 katika mechi 109 alizoichezea nchi hiyo, na kumfanya kuwa mfungaji bora wa muda wote wa Ghana.
“Will never leave my love “ ❤️⚽️ @ghanafaofficial @CAF_Online @FIFAWorldCup @FIFAcom @AnimSammy @PrinxRandy pic.twitter.com/IX05ZTywlw
— ASAMOAH GYAN (@ASAMOAH_GYAN3) June 20, 2023
Mchezaji huyo mwenye umri wa miaka 37 alianza maisha yake ya soka mwaka 2003 akichezea timu ya kwanza ya Ghana, Liberty Professionals, na baadaye akachezea Udinese ya Serie A nchini Italia, Rennes ya Ligi Kuu ya Ufaransa na Sunderland ya Ligi Kuu ya Uingereza, ambapo alivunja rekodi ya uhamisho wa klabu hiyo.
Aliwahi kucheza katika Falme za Kiarabu, akiichezea Al Ain, akiisaidia timu hiyo kushinda taji la Ligi ya UAE na kuwa mfungaji bora wa ligi hiyo akiwa amefunga mabao 28 katika mechi 32. Pia alichezea Shanghai SIPG, Kayserispor na North East United.
Akiwa nyumbani kwao Ghana, Gyan aliichezea timu ya taifa ya wakubwa, Black Stars, katika Kombe la Dunia la Fifa mara tatu - mwaka wa 2006, 2010 na 2014. Ndiye mfungaji bora wa Kombe la Dunia barani Afrika, akiwa na jumla ya mabao sita.
Aliichezea nchi yake katika michuano saba ya Kombe la Mataifa ya Afrika, ambapo Black Stars ilimaliza nafasi ya tatu mwaka wa 2008 na katika nafasi za pili mwaka wa 2010 na 2015.
Gyan alitumia siku zake za mwisho za maisha ya soka akichezea Legon Cities FC ya nchini Ghana. Pia alitoa memoir yenye jina LeGYANDry, akielezea maisha yake na safari ya soka.