Pata taarifa kuu

Waamuzi wa michuano ya robo fainali klabu bingwa na Shirikisho wafahamika

NAIROBI – Na Mchambuzi wetu Paul Nzioki

Kikosi cha wachezaji wa klabu ya Yanga ya nchini Tanzania
Kikosi cha wachezaji wa klabu ya Yanga ya nchini Tanzania © Young Africans
Matangazo ya kibiashara

Shirikisho la Soka barani Afrika (CAF) limemteua mwamuzi kutoka taifa la CHAD Alhadi Allaou Mahamat kuchezesha mchezo kati ya Simba SC ya Tanzania na Wydad Club Athletic ya Morocco.

Mechi hii itakua ya mkondo wa pili katika mechi za kuwania ubingwa wa vilabu barani Afrika.

Simba itashuka dimbani kesho Jumamosi saa tisa alasiri kwa saa za Afrika Mashariki kwenye Uwanja wa Stade Mohamed V (Maarufu Mohammed Wa Tano) mjini Casablanca, Morocco.

Mechi ya simba dhidi ya Wydad Athletic Club
Mechi ya simba dhidi ya Wydad Athletic Club © simba
Kwa mujibu wa taarifa ya CAF, Mahamat atasaidiwa na Elvis Guy Noupue Nguegoue kutoka Cameroon na Issa Yaya, pia kutoka Chad huku afisa wa nne akiwa Mahmood Ali Mahmood Ismail kutoka nchini Sudan.

Simba ilishinda bao 1-0 katika mchezo wa kwanza uliochezwa katika Uwanja wa Benjamin Mkapa (Maarufu Estadio De Benjamin Mkapa) jijini Dar es Salaam.

Mashabiki wa Simba ya nchini Tanzania
Mashabiki wa Simba ya nchini Tanzania © simba
Wekundu wa Msimbazi wanahitaji sare pekee wakiwa ugenini kuvunja mwiko wa kutofuzu katika hatua ya nusu fainali katika mashindano ya CAF ya hivi karibuni.

Hata hivyo, Simba itakosa huduma za wachezaji wake watatu, Mlinda lango Aishi Manula ambaye anauguza jeraha , Augustine Okrah na Mohamed Ouattara.

Kocha mkuu wa timu hiyo, Roberto Oliveira Gonçalves do Carmo maarufu kama Robertinho, alisema wataenda kuthibitisha thamani yao katika pambano hilo licha ya kukabiliwa na kibarua kigumu.

Wakati huo huo, mchezo wa marudiano wa hatua ya robo fainali ya michuano ya Kombe la Shirikisho Afrika kati ya Yanga na Rivers United, utachezeshwa na waamuzi kutoka nchini Morocco.

Kwa mujibu wa taarifa ya CAF, Redouane Jiyed atakuwa katikati ya uwanja katika pambano hilo ngumu.

Wachezaji wa Yanga baada ya ushindi wao dhidi ya Rivers united ya nchini Nigeria
Wachezaji wa Yanga baada ya ushindi wao dhidi ya Rivers united ya nchini Nigeria © Young Africans
Jiyed atasaidiwa na Lahcen Azgaou na Mostafa Akarkad huku mwamuzi wa akiba akiwa ni Jalal Jayed, pia kutoka Morocco.

Young Africans wanahitaji sare yoyote ili kuweka historia ya kutinga hatua ya nusu fainali ya michuano hiyo na wao pia kuvunja mwiko wa timu za Tanzania kutoshiriki hadi nusu fainali katika michuano ya CAF.

Wananchi walipata ushindi wa 2-0 ugenini katika uwanja wa Goodwill Akpabio kule Nigeria.

Wachezaji wa Wydad Club Athletic ya Morocco
Wachezaji wa Wydad Club Athletic ya Morocco © wydad club Athletic
Licha ya ushindi wa mabao 2-0 ugenini, Kocha Mkuu wa Yanga, Nasreddine Nabi, alisema wanaichukulia kwa uzito mchezo huo nawanalenga ushindi ili kutinga nusu fainali ya michuano hiyo ya kifahari Afrika.

Wachezaji wa Yanga wameanza mazoezi jana kujiandaa na mchezo huo unaotarajiwa kuanza saa 7 mchana Jumapili kwenye Uwanja wa Benjamin Mkapa.

Kusambaza :
Ukurasa haipatikani

Maudhui unayojaribu kuyatafuta hayapatikani kwa sasa au yamekwishaondolewa.