Manchester City yaicharaza Bayern Munich robo fainali ya UEFA
NAIROBI – Na Jason Sagini
Imechapishwa: Imehaririwa:
Mshambuliaji wa Manchester City, Erling Haaland, kutoka Norway anazidi kung’ara baada ya kuisaidia City kuilaza Bayern Munich magoli 3-0 ugani Etihad Jumanne usiku katika mchezo wa robo fainali ya ligi ya mabingwa bara ulaya.
Haaland alifunga bao moja katika dakika ya 76 baada ya kuandaa bao la Bernado Silva dakika ya 70. Kufuatia magoli hayo, Haaland sasa amepachika magoli 45 na kuvunja rekodi ya mholanzi Ruud van Nistelrooy na raia wa Misri Mohammed Salah ya magoli 44 katika mashindano yote kwenye msimu mmoja.
Aidha, alifanikiwa kusajili ushindi wa kwanza dhidi ya Bayern Munich baada ya ukame wa mechi saba dhidi ya klabu hiyo ya Ujerumani.
Romelu Lukaku na Nico Barella waliifungia Inter Milan katika ushindi wa 2-0 ugenini dhidi ya Benfica. Hiki ni kipigo cha kwanza msimu huu kwa Benfica katika ligi hii baada ya kupokea kichapo cha kwanza katika uwanja wao wa nyumbani wa Estádio da Luz siku ya Ijumaa wiki iliyopita dhidi ya Porto.
Jumatano usiku, mabingwa mara kumi na nne Real Madrid watawakaribisha mabingwa mara mbili Chelsea ugani Santiago Bernabeau wakati AC Milan mabingwa mara saba watawakaribisha Napoli ambao wanasaka ubingwa wao wa kwanza.
Kwa msimu wa tatu mfulilizo, Real Madrid na Chelsea zitakutana kwenye hatua ya muondoano ambapo mshindi wa mechi hii alimaliza mashindano kama bingwa kwa misimu miwili waliyokutana awali. Timu zote hizi hazifanyi vizuri katika ligi zao za nyumbani haswa baada ya kupoteza mechi zao za wikendi iliyopita – kwa hivyo wote wataweka nguvu zao zote kupigania kombe hili.
Milan dhidi ya Napoli ni robo fainali nyingine ya kusisimua kwani hizi ni timu mbili kati ya tatu kutoka Italia zilizosalia mashindanoni na watakutana kwa mara ya kwanza kabisa kwenye ligi hii. AC Milan ambayo ilifuzu kwenye hatua hii ya muondoano kwa mara ya kwanza baada ya miaka 11, italenga ushindi katika mchezo huu wa nyumbani ila rekodi yao mbovu uwanjani San Siro ya ushindi mara moja tu kati ya mechi tisa zilizopita huenda itawaponza dhidi ya viongozi wa ligi ya Serie A , Napoli.
Napoli iliishinda Milan nyumbani kwao magoli 2-1 katika mchezo wa ligi ya Italia mkondo wa kwanza wakati Milan iliipiga Napoli magoli 4-0 katika mchezo wa marudiano.