Uchambuzi: Hatima ya soka la wanawake katika nchi za Afrika Mashariki
Na: Mchambuzi wetu Jason Sagini
Imechapishwa: Imehaririwa:
Milioni moja hujazwa kwa kuunganisha shilingi moja baada ya nyingine. Cha muhimu zaidi ni bidii na utendakazi wako katika kukusanya shilingi zako moja kila kuchao.
Soka la wanaume limekua na linakua kwa kasi zaidi tangua miaka ya 1900. Tunazungumzia mabadiliko kiteknolojia na kuiboresha kibiashara kwa kuunda ligi zenye vilabu na timu bora duniani (Ligi ya Supa, Ligi ya Afrika, UEFA Nations).
Nini kinachangia ukuaji wa soka la wanawake katika ukanda wa Afrika Mashariki kushikwa na kigugumizi ? Ni mjadala mrefu.
Mwaka 2020, baada ya kushinda kombe la dunia la wanawake, mshambulizi wa Marekani Megan Rapinoe alijitokeza na kudai wachezaji wa kike wanapswa kupokea mishahara sawa na wanaume.
Mwaka 2018, ligi kuu ya Ufaransa ya kina dada ilikua inaongoza kulipa wachezaji wake mshahara wastani wa ($49,782) kwa mwaka ikifuatwa na Ujerumani ($43,730) ambapo wanaume wa Ujerumani walipokea wastani wa euro milioni 1.4.
Mwezi Septemba mwaka 2020, shirikisho la soka Uingereza lilifichua kuwa ilianza kuwalipa wachezaji wa timu ya taifa kwa jinsia zote kwa usawa tangu mwezi Januari 2020. Hili liliungwa mkono na mataifa mengine kama vile Australia, New Zealand na Norway.
Afrika Mashariki, mwezi Julai mwaka 2020, shirikisho la soka nchini Kenya (FKF) lilipotia saini mkataba wa udhamini (bilioni 1.2) wa miaka mitano na kampuni ya uwekezaji kutoka Nigeria, vilabu za wanaume zingepokea milioni nane za Kenya kila mwaka.
Ligi kuu ya wanawake (sio vilabu) ingepokea milioni kumi na mbili ambayo ni ada ya leseni kwa mwaka inayotozwa kwa vilabu vya wanaume ligi kuu. Usawa unakua changamoto na inabidi mmoja ale mabaki kama njia ya kumliwaza.
Kwenye upeperushaji wa mechi. Mwezi Novemba mwaka 2020 FKF iliingia kwenye makubaliano ya miaka saba na kampuni ya Startimes kupeperusha mechi za ligi kuu, thelathini za ligi ya daraja la pili na mechi za kirafiki za Harambee Stars.
Ligi ya kina dada wala Harambee Starlets haikutajwa. Kwa aina fulani kunakosekana usawa katika udhamini na maslahi ya ligi ya wanaume na kina dada.
Wapiganapo fahali wawili ...? Majuzi tu timu ya taifa ya kina dada ya Kenya (Harambee Starlets) ilifungiwa kushiriki hatua ya mwisho kufuzu mashindano ya kombe la mataifa bingwa Afrika baada ya mkurugenzi wa FKF, Barry Otieno kuandikia shirikisho la soka Afrika (CAF) kuwa hawana uwezo wa kuandaa mechi dhidi ya Uganda.
Hii ni baada ya FKF kufurushwa ofisini kwa nguvu na waziri wa michezo Amina Mohammed kwa madai ya ufisadi. Vuta nikuvute hiyo ilipelekea talanta za wachezaji wa kike kuyumbishwa na kukosa nafasi hiyo adimu ya kujiuza haswa baada ya kuishinda Sudan mabao 15-1 katika raundi ya kwanza.
Mchezo wa soka umehusishwa na mtoto wa kiume mara nyingi kwa kina dada ukihusishwa kimaumbile. Ashakum si matusi, jamii ina mtazamo kuwa dada anayecheza soka si mtoto wa kike bali wa kiume na kuolewa kwake itakua ndoto ya mchana.
Matamshi kama haya haswa kutoka kwa viongozi wetu yatazamisha kabisa juhudi za kuinua soka ya kina dada na kuwafanya dada zetu kufa moyo maana jamii ni ya waasi tayari. Kama una muda tembea Uhabeshi mtazame Lorza Geinore, mshambulizi wa klabu ya
CBE, Corazone Aquino na Esse Akida huko Kenya . Tuache dhana hii potovu na tuonyeshe kuwaunga mkono kutia fora.
Ukosefu wa washikadau wa kutosha katika soka la kina dada pia linachangia kukua kwa kujikokota sababu hakuna anayetetea na kusukuma ajenda za kike. Umoja ni nguvu, kidole kimoja hakivunji chawa. Makocha, marefari, wasimamizi, mawakala hata wanahabari wa michezo wa kike ni wachache ikilinganishwa na wa kiume.