Mataifa ya Afrika kujitupa viwanjani kutafuta tiketi ya kufuzu kucheza AFCON 2019
Jumamosi na Jumapili kutakuwa na michuano kadhaa ya soka, hatua ya makundi, kutafuta nafasi ya kufuzu fainali ya bara Afrika mwaka 2019 nchini Cameroon.
Imechapishwa:
Nchini Kenya, Harambee Stars itakuwa nyumbani kucheza na Black Stars ya Ghana, katika mechi ya kundi F.
Mechi hii itachezwa katika uwanja wa Moi Kasarani. Kenya itakuwa bila ya nahodha wake wa siku nyingi Victor Wanyama anayecheza soka ya kulipwa katika klabu ya Tottenham Hotspurs kwa sababu anauguza majeraha.
Nchini Uganda, Cranes watakuwa wenyeji wa Taifa Stars ya Tanzania katika uwanja wa Namboole jijini Kampala.
Tanzania wanakwenda katika mchuano huu wa kundi L wakiwa na kocha mpya Emmanuel Amunike, na wengi wanasubiri kuona kibarua chake cha kwanza hapo kesho kitakuwa vipi.
Jijini Libreville, wenyeji Gabon watawakaribisha Burundi huku mabingwa watetezi Cameroon wakiwa mjini Moroni kucheza na Comoros.
Mechi zingine za Jumamosi:- Ushelisheli vs Nigeria, Namibia dhidi ya Zambia, Equitorial Guinea vs Sudan na Misri dhidi ya Niger.
Siku ya Jumapili, Rwanda itakuwa jijini Kigali kucheza na Cote Dvoire, Liberia itakuwa wenyeji wa Jamhuri ya Kidemokrasia ya congo, huku Sudan Kusini wakicheza na Mali.
Hii ni michuano ya mzunguko wa pili, na michuano hii inachezwa nyumbani na ugenini.
Tukisalia barani Afrika, mechi za kufuzu katika fainali ya Afrika kwa vijana wasiozidi miaka 17 kwa ukanda wa Afrika Magharibi inaendelea.
Fainali hii itafanyika nchini Tanzania mwaka ujao, siku ya Jumamosi Togo itacheza na Ghana lakini Jumapili, Mali itamenyana na Gambia huku Mauritania ikimenyana na Guinea.