Essam El Hadary aweka rekodi kombe la dunia
Kipa wa kimataifa wa Misri Essam El Hadary ameweka rekodi ya kuwa mchezaji mwenye umri mkubwa kucheza fainali za Kombe la dunia.
Imechapishwa:
Golikipa huyo anayechezea klabu ya Al-Taawoun mkongwe ana umri wa miaka 45 na siku 161 na ameichezea Misri maarufu kama Pharaos zaidi ya mechi 150.
Kipa huyo aliyeshinda mataji matatu ya Afrika atakaa langoni wakati Misri itakapochuana na Saudi Arabia katika mchezo wa kukamilisha ratiba wa Kundi A, Misri imeshaondolewa mashindanoni baada ya kushindwa katika michezo miwili ya awali.
“Umri wangu ni miaka 45 lakini kwa mtazamo wangu hizi ni namba tu. Baba yangu alifariki lakini ndoto yake ilikuwa ni kuniona nikicheza fainali za Kombe la dunia. Nataka kumpa furaha baba yangu,”amesema Hadary, alipohojiwa na BBC