Serikali nchini Ugiriki yasimamisha ligi kuu ya soka
Ligi kuu ya soka nchini Ugiriki imesitishwa kwa muda usiojulikana baada ya Mwenyekiti wa klabu ya PAOK kuvamia eneo la kuchezea akiwa na bastola.
Imechapishwa:
Naibu wa Michezo nchini humo Yiorgos Vassiliadis, amesema uamuzi huu umefikiwa baada ya kukutana na kufanya kikao cha dharura na Waziri Mkuu Alexis Tsipras kutokana na tukio hilo.
Serikali nchini Ugiriki inataka sera mpya ya soka kukubaliwa na wadau wote nchini humo kwa ushirikiano na Shirikisho la soka barani Ulaya UEFA, kabla ya kurejelewa kwa ligi hiyo.
Hati ya kukamatwa imetolewa kwa Mwenyekiti wa klabu hiyo ya PAOK, Ivan Savvidis mfanyibiashara na mwanasiasa mwenye asili ya Urusi ambaye aliingia eneo la kuchezea akiwa na bastola.
Savvidis alikwenda kumlalamikia mwamuzi baada ya kukataa bao lililokuwa limefungwa na klabu yake katika dakika ya 90 dhidi ya klabu ya AEK Athens.
Baada ya majibizano makali, mwamuzi huyo aliamua kukubali shinikizo na kuipa PAOK bao hilo.
Timu hizo mbili PAOK na AEK pamoja na Olympiakos Piraeus ziko mbioni kutafuta ubingwa soka nchini humo. .