Guinea yailemea Senegal kufuzu fainali ya CHAN
Timu ya taifa ya soka ya Guinea iliishinda Senegal mabao 5-0 katika mchuano muhimu wa kufuzu fainali ya CHAN, kwa wachezaji wanaocheza soka nyumbani, itakayofanyika mwaka ujao nchini Kenya.
Imechapishwa:
Mshambuliaji Amadou Sekou Camara ndiye aliyekuwa nyota wa mchezo huo baada ya kufunga mabao 3 katika mchuano huo uliochezwa usiku wa kuamkia leo jijini Conakry.
Guinea sasa inaugana na mataifa 15 wakiwemo wenyeji Kenya katika fainali hiyo.
Mataifa mengine yaliyofuzu ni pamoja na wenyeji:- Kenya, Libya, Morocco, Uganda, Ivory Coast, Mauritania, Sudan, Nigeria, Zambia, Equatorial Guinea, Congo, Cameroon, Angola, Namibia, Burkina Faso na Guinea.
Wakati uo huo maafisa wa Shirikisho la soka barani Afrika CAF, wanatarajiwa kuzuru Kenya wiki ijayo kujionea maandalizi ya michuano hiyo.
Kumekuwa na ripoti kuwa huenda Kenya itapoteza nafasi hiyo ikiwa hali ya viwanja nchini humo haitawaridhisha wakaguzi wa CAF, na labda michuano hiyo kupelekwa nchini Morocco, Zambia au hata Afrika Kusini.