Serena atupwa nje US Open, kupoteza nafasi ya kwanza kwa Kerber
Mchezaji Karolina Pliskova raia wa Jamhuri ya Czech anayeshikilia nafasi ya 10 kwa ubora wa mchezo wa tenesi, amefanikiwa kumfunga Serena Williams na kutinga hatua ya fainali ya michuano ya US Open na kumaliza utawala wa mchezaji huyo kuwa nambari moja duniani.
Imechapishwa:
Serena mwenye umri wa miaka 34 hivi sasa, alijikuta akifanya makosa ya kizembe yaliyosababisha ajikute akipoteza mchezo wake kwa matokeo ya seti 6-2, 7-6 na 7-5, matokeo ambayo sasa yanamfanya Pliskova kukutana na Mjerumani Angelique Kerber anayeshika nafasi ya pili kwenye mchezo wa fainali.
Matokeo haya pia yanamaanisha kuwa Kerber atashika nafasi ya kwanza kwa ubora wa mchezo huo upande wa wanawake baada ya kumalizika kwa michuano ya US Open akimpiku Serena.
Serena alikuwa akilenga kuwania taji lake la 23 la michuano mikubwa ya tenesi ili aweke rekodi, lakini akajikuta ndoto zake zikizimwa na Pliskova.
Hata hivyo anaendelea kusalia na rekodi sawa na mchezaji tenesi mashuhuru Steffi Graf ambao wote wanashikilia rekodi moja ya kutwaa mataji makubwa kwa upande wa mchezaji mmoja mmoja pamoja na taji la WTA kwa rekodi ya wiki 186 kuwa nambari moja duniani.
Akuzungumza mara baada ya mchezo wake, Serena amemsifu Pliskova, ambaye amesema alicheza vizuri na kukiri kuwa majeraha ya goti lake pia yalichangia kumfanya ashindwe kuwa kwenye kiwango bora.
Bingwa wa taji la Australian Open Mjerumani Angelique Kerber alimfunga Carolina Wozniacki raia wa Denmark kutinga hatua ya fainali kwa kumfunga kwa seti mbili bila kwa matokeo ya 6-4 na 6-3.