Ubelgiji kusaka ushindi muhimu kufuzu hatua ya 16 bora
Ni Jumamosi nyingine ya michuano ya soka hatua ya makundi kuwania ubingwa wa bara Ulaya.
Imechapishwa:
Michuano hii inaendelea katika viwanja mbalimbali nchini Ufaransa.
Ubelgiji inafungua dimba katika mchuano wake wa pili wa kundi E dhidi ya Jamhuri ya Ireland kuanzia saa 10 jioni saa za Afrika Mashariki.
Ubelgiji ilipoteza mechi yake ya kwanza dhidi ya Italia kwa kufungwa mabao 2 kwa 0.
Italia tayari imefuzu katika hatua ya 16 bora baada ya kuishinda Sweden bao 1 kwa 0 siku ya Ijumaa na sasa Ubelgiji inahitaji ushindi leo ili kujihakikishia nafasi ya kufuzu katika hatua ya mwondoano.
Iceland nayo itavaana na Hungary katika mchuano wa pili wa kundi la F kuanzia saa Moja jioni, saa za Afrika Mashariki.
Hungary inaongoza kundi hili kwa alama 3 baada ya kupata ushindi wake wa kwanza dhdi ya Austria wa mabao 2 kwa 0.
Iceland ilianza michuano hii kwa kutoka sare ya bao 1 kwa 1 na Ureno.
Mchuano wa mwisho leo Jumamosi ni kati ya Ureno na Austria kuanzia saa nne usiku saa za Afrika Mashariki.
Kesho Jumapili:-
Uswizi vs Ufaransa
Romania vs Albania.
Mechi za kumaliza kundi A zitachezwa kuanzia saa nne usiku saa Afrika Mashariki.
Hadi sasa mataifa ambayo yamefuzu katika hatua ya 16 bora ni pamoja na wenyeji Ufaransa, mabingwa watetezi Uhispania na Italia.
Mechi ya fainali itachezwa tarehe 10 mwezi ujao jijini Paris.