UEFA yaanza uchunguzi dhidi ya mashabiki wa Urusi
Kamati ya Shirikisho la soka barani Ulaya UEFA limeanza uchunguzi wa kina baada ya mashabiki wa timu ya taifa ya Urusi kuwashambulia mashabiki wa Uingereza wakati nchi hizo zilipokabiliana katika mchuano wao wa kwanza wa kundi B, kuwania taji la bara Ulaya siku ya Jumamosi.
Imechapishwa:
Kanda za video zimeonesha mashabiki wa Urusi wakiwakimbilia wale wa Uingereza na kuanza kuwashambulia baada ya mechi kukamilika kwa sare ya bao 1 kwa 1 mjini Marseille.
UEFA inasema itaichukua Urusi hatua baada ya mashabiki wake kuzua fujo, kuonesha vitendo vya ubaguzi wa rangi na kutumia fataki kuwashambulia mashabiki wa Uingereza.
Waziri wa Michezo wa Urusi Vitaly Mutko amenukulia akisema anaunga mkono uchunguzi wa UEFA na kusisitiza kuwa tabia ya mashabiki wa nchi yake haikubaliki katika mchezo wa soka.
Mashabiki wa mataifa hayo mawili pia walikabiliana nje ya uwanja na polisi wa kutuliza ghasia wakalazimika kutumia mabomu ya kutoa machozi kuwasambaratisha.
UEFA inatarajiwa kutangaza vikwazo dhidi Shirikisho la soka la Urusi siku ya Jumanne juma lijalo.
Hii sio mara ya kwanza kwa mashabiki wa Urusi kujikuta katika hali kama hii, mwaka 2012 wakati michuano hii ilipofanyika Poland na Ukraine, Shirikisho la soka nchini humo lilitozwa fainai ya Euro 190,000 kwa sababu ya fujo za mashabiki wake.
Matokeo Kamili ya Kundi B
Wales 2-1 Slovakia
Uingereza 1-1 Urusi
Wales inaongoza kundi hili kwa alama 3, ikifuatwa na Uingereza kwa alama 1, Urusi ni ya nne kwa alama 1 huku Slovakia ikiwa ya mwisho bila ya alama.
Mechi zijazo Juni 15 2016
Urusi vs Slovakia
Juni 16 2016
Uingereza vs Wales