Sulley Muntari na Kevin-Prince Boateng wafukuzwa kambini
Wachezaji wa Kimataifa wa timu ya taifa ya Ghana Sulley Muntari na Kevin-Prince Boateng wamefukuzwa katika kambi ya timu hiyo nchini Brazil kwa sababu za kinidhamu.
Imechapishwa:
Shirikisho la soka nchini Ghana, limethibitisha kufuzwa kwa wawili hao ambao walikuwa katika kikosi cha “ The Black Stars” na kushiriki katika michuano miwili iliyopita.
Shirikisho hilo linasema Boateng alitumia maneno makali na ya kumkejeli kocha Kwesi Appiah huku Muntari akimvamia na kumjeruhi afisa wa Kamati ya shirikisho la soka GFA.
Wawili hao wanarudi nyumbani muda mfupi tu kabla ya Ghana kuvaana na Ureno katika mchuano muhimu wa kuamua ikiwa watasonga mbele katika michuano hiyo au la, Alhamisi usiku.
Aidha, Shirikisho la soka la Ghana linasema Muntari anayechezea soka la kulipwa katika klabu ya AC Milan nchini Italia alimjeruhi afisa wa Kamati ya shirikisho hilo aliyefahamika Moses Armah siku ya Jumanne wakiwa kambini.
Shirikisho hilo linasema Boateng ambaye anaichezea Schalke 04 ya Ujerumani hakuomba msamaha wala kusikitika baada ya kumtusi kocha wake wakiwa kambini.
Juma hili, kambi ya Ghana ilikuwa baridi baada ya wachezaji kukataa kutumiwa marupurupu yao kutoka Accra na kuilazimisha serikali kukodi ndege maalum na kusafirisha zaidi ya Dola Millioni 3 fedha taslimu kuwalipa wachezaji hao.
Mbali na hilo, kulitokea na madai kuwa Shirikisho la soka la Ghana lilikuwa linapanga matokeo baada ya michuano ya kombe la dunia, kwa mujibu wa uchunguzi wa gazeti la Uingereza la The Telegraph.