Kocha wa timu ya taifa ya Uingereza kutangaza kikosi chake hii leo, kumuacha Cole
Kocha mkuu wa timu ya taifa ya Uingereza Roy Hodgson hii leo anatarajiwa kutangaza kikosi cha wachezaji wake 23 ambao watashiriki fainali za kombe la dunia mwaka huu nchini Brazili.
Imechapishwa: Imehaririwa:
Kocha Roy Hodgson pia anatarajiwa kutangaza wachezaji saba ambao watakuwa kwenye orodha ya akiba na ambao wataitwa iwapo moja kati ya wachezaji wake 23 atakaowatangaza ataumia wakati michuano hiyo ikiendelea.
Kocha huyu anatarajiwa kutangaza kikosi ambacho huenda kikasheheni wachezaji makinda zaidi ambao ndio watakaopewa nafasi kwenye kikosi cha Uingereza kitakachoshiriki michuano ya mwaka huu.
Katika hatua nyingine, beki wa kushoto wa klabu ya Chelsea na Uingereza, Ashley Cole hatimaye ametangaza kustaafu kuitumikia timu yake ya taifa baada ya kupokea simu toka kwa kocha wake Roy Hodgson akimtaarifu kuwa hatamjumuisha kwenye kikosi chake.
Akiandika kwenye mtandao wa kijamii wa Twitter, Cole anasema "Kocha wangu ameinipigia simu kunitaarifu kuwa hatanijumuisha kwenye kikosi chake atakachokitangaza na kwamba nimekubaliana nae kuwa ni lazima vijana wapewe nafasi kwenye timu hiyo" anasema Cole.
Beki huyo ambaye ameitumikia timu ya taifa ya Uingereza kwa miaka kadhaa, amekuwa hana namba sana kwenye klabu yake ya Chelsea na hivyo kushindwa kuthibitisha makali yake ambayo huenda kocha wake Hodgoson angezingatia kwa kumuita kwenye timu yake.