Malaga yadhamiria kuiangamiza Milan katika mechi ya Jumanne
Timu ya soka ya Malaga ya nchini Ufaransa inashuka dimbani Jumanne hii kutafuta pointi tatu muhimu dhidi ya mahasimu wao AC Milan katika moja ya mechi ya ligi ya mabingwa barani Ulaya msimu huu zinazoendelea kutimua vumbi katika viwanja mbalimbali barani humo.
Imechapishwa: Imehaririwa:
Kocha wa Malaga ambaye ni raia wa Uhispania Manuel Pellegrini amejigamba kuwa ni lazima waibuke na ushindi hivyo wapinzani wao wajiandae kupokea kichapo cha nguvu zaidi ya kile walichokipata katika mechi ya awali.
Malaga imekuwa ikifanya mashambulizi ya kushtukiza katika mashindano ya msimu huu na kufanikiwa kuibuka na ushindi katika mechi zao zote tatu ambazo ni pamoja na goli moja kwa bila waliloifunga Milan katika mechi yao ya awali iliyopigwa mwezi uliopita.
Mpaka sasa Malaga ipo kileleni katika kundi C nafasi ambayo ilichangiwa kwa kiasi kikubwa na matokeo waliyoyapata katika mechi yao dhidi ya Milan ya mwezi uliopita.
Pellegrini ameongeza kuwa kikosi chake kimejipanga kuchukua ubingwa msimu huu hivyo hawatakubali kichapo cha mbwa mwizi kama Chievo ambayo ilipachikwa magoli 5-1 na Milan katika mechi zilizopigwa mwishoni mwa juma lililopita.