Watu 9 wamepoteza maisha katika shambulio la bomu nje ya mahakama kuu ya jijini New Delhi, India
Watu tisa wamedhibitishwa kufa na wengine zaidi ya arobaini na tano wamejeruhiwa nchini India baada ya kutokea mlipuko wa bomu nje ya jengo la mahakama kuu ya nchi hiyo mjini New delhi.
Imechapishwa:
Kamishna wa kikosi maalumu cha Polisi mjini New Delhi, Dharmendra Kumar amewaambia waandishi wa habari kuwa uchunguzi wa awali umeonyesha kuwa bomu hilo lilihifadhiwa katika Briefcase na kuwekwa katika lango kuu la kuingilia mahakamani hapo.
Msemaji wa wizara ya mambo ya ndani RK Singh amedhibitisha kutokea kwa shambulio hilo la bomu na kuongeza kuwa mpaka sasa ni watu tisa wamepoteza maisha na wengine zaidi ya arobaini na tano wamejeruhiwa katika tukio hilo.
Polisi wamesema kuwa mpaka sasa hakuna kikundi chochote cha watu kilichokiri kuhusika na shambulio hilo na kwamba uchunguzi bado unaendelea kubaini watu waliotekeleza shambulio hilo.
Hili ni shambulio jingine la pili kutekelezwa nje ya jengo la mahakama kuu ya nchi hiyo kufuatia mlipuko mwingine wa bomu uliotokea mwezi wa sita mwaka huu na kujeruhi watu kadhaa.