Pata taarifa kuu
SUDAN KUSINI-MACHAR-KIIR-AMANI

Rais Kiir asema vita vimeisha Sudan Kusini

Rais wa Sudan Kusini Salva Kiir, amesema vita vimemalizika nchini humo na sasa kazi inayosalia ni kuliunganisha upya na kuhubiri maridhiano katika taifa hilo changa, lililopata uhuru mwaka 2011.

Salva Kiir na Riek Machar wakisalimiana mwezi Septemba 2018
Salva Kiir na Riek Machar wakisalimiana mwezi Septemba 2018 YONAS TADESSE / AFP
Matangazo ya kibiashara

Rais Kiir ametoa kauli hiyo siku ya Jumatano, wakati wa sherehe za kuadhimisha upatikanaji wa mkataba wa amani jijini Juba.

Mkataba huo ulitiwa saini mwezi Septemba jijini Khartoum nchini Sudan na kushuhudiwa na viongozi wa ukanda wa IGAD chini ya rais Omar Al Bashir.

“Nataka nisisitize mbele yenu na mbele ya wageni hawa kutoka maeneo mbalimbali ya dunia kuwa, vita vimefika mwisho, Dokta Machar na mimi na viongozi wengine wa upinzani waliotia saini makata hay, tumesameheana na kuamua kusonga mbele na kuanza mchakato wa uponyaji,” alisema rais Kiir huku akipigiwa makofi.

Aidha, Kiir ameomba msamaha kwa wananchi wa taifa hilo kwa kile alichosema, vita hivyo vilikuwa vya kisiasa na wala sio vya wananchi.

“Naomba msamaha, hivi ni vita ambavyo vilikuwa vya kisiasa, havikuwa vya wananchi,” aliongeza.

Kwa upande wake, kiongozi wa upinzani na waasi Riek Machar, amesisitiza kuwa ana nia ya dhati ya kuhakikisha kuwa amani inarejea.

Imekuwa ni kwa mara ya kwanza kwa Machar kurejea nchini kwa mara ya kwanza ndani ya miaka miwili, baada ya vita kutokea mwaka 2016 jijini Juba.

Sherehe hizo zilihuhudhuriwa na viongozi wa ukanda kutoka Ethiopia, Somalia huku mataifa mengine yakituma wawakilishi.

Rais wa Uganda Yoweri Museveni, ametoa wito kwa raia na viongozi wa Sudan Kusini, walinde amani waliyopata.

“Nawapongeza sana kwa amani hii, na watu wote wa Sudan Kusini na wadau sasa waweke maagano kama walivyofanya watoto wa Israel walipopata sheria kumi za Mungu katika Mlima Sinai, na agano muhimu liwe ni kuwa hakuna vita vitakavyofanyika kutatua migogoro ya kisiasa, “ alisema rais Museveni.

Waangalizi wa siasa za Sudan Kusini wanasubiri kuona iwapo mkataba huo utatekelezwa kikamilifu.

Kusambaza :
Ukurasa haipatikani

Maudhui unayojaribu kuyatafuta hayapatikani kwa sasa au yamekwishaondolewa.