Njaa na kipindupindu vyatishia wakaazi mashariki mwa DRC
Maelfu ya makazi madogo ya muda yamekusanyika kando ya barabara kaskazini mwa mji wa Goma mashariki mwa Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo, mashahidi wa mgogoro mkubwa wa kibinadamu unaoendelea katika eneo hili lenye migogoro.
Imechapishwa:
Makumi kwa maelfu ya wakaazi wa eneo la Rutshuru wametoroka makaazi yao tangu mwishoni mwa mwezi Oktoba hadi eneo la usalama la mji mkuu wa mkoa wa Kivu Kaskazini, wakikimbia waasi wa M23.
Walio hatarini zaidi wanaishi kando ya barabara, katika vibanda vilivyofunikwa na turubai, kwenye uwanja wa lava ngumu chini ya volkano ya Nyiragongo.
Licha ya uingiliaji kati wa mashirika ya kibinadamu, watu wote waliokimbia makazi waliohojiwa na shirika la habari la AFP wanalalamikia njaa. Wengi wanaripoti kwamba wanapaswa kupigana ili kupata chakula. Na kipindupindu, athari ya ukosefu wa usafi, kimeripotiwa.
Kundi la M23, ambalo wengi wao ni waasi wa Kitutsi walioshindwa mwaka 2013, walichukua tena silaha mwishoni mwa mwaka jana.
Mnamo mwezi Juni liliteka Bunagana, kwenye mpaka wa Uganda, kisha, baada ya utulivu, liliendelea na mashambulizi tena mwezi wa Oktoba, na kukamata maeneo makubwa ya kaskazini mwa Goma na kusababisha maelfu ya watu kutoroka makazi yao.