Rais Putin anazuru China
Nairobi – Rais wa Urusi Vladimir Putin amewasili nchini China kukutana na “rafiki wake mkuu” rais Xi Jinping, ziara inayolenga kuimarisha uhusiano kati ya mataifa hayo mawili.
Imechapishwa:
China wiki hii inatarajiwa kuwa mwenyeji wawakilishi kutoka katika mataifa 130 ya dunia, katika kongamano rais Xi kuhusu biashara na miundo mbinu na masuala ya barabara.
Kongamano hili linafanyika wakati huu mapigano yakiendelea kuripotiwa kati ya wanajeshi wa Israeli na wapiganaji wa Hamas.
Rais Putin ni miongoni mwa wageni wa ngazi ya juu kwenye kongamano hilo, hii ikiwa ni ziara yake ya kwanza kwenye taifa lenye uchumi mkubwa tangu nchi yake kuivamia Ukraine.
Tangu uvamizi huo, Urusi imeonekana kutengwa na baadhi ya mataifa ya dunia katika majukwa ya kimataifa.
Putin anatarajiwa kufanya mazungumzo na mwenyeji wake rais Xi pembezoni ya mkutano huo wa Jumatano ya wiki hii.
Kremlin imesema suala la Israeli na Hamas pia litapewa nafasi katika kongamano hilo.
Mataifa ya Magharibi yakiongozwa na Marekani yameonekana kuunga mkono Israeli tangu Hamas kutekeleza shambulio mbaya zaidi katika historia dhidi yake.
Marekani ilitoa wito kwa China kutumia ushawishi wake kusaidia kumaliza mzozo ambao umesababisha zaidi ya raia milioni moja katika ukanda wa Gaza kutoroka mapigano na mashambulio ya Israeli.
Rais Xi alifungua kongamano hilo siku ya Jumanne kwa kufanya mazungumzo na marais wa Chile na Kazakhstan kwa mujibu wa shirika la habari linalomilikiwa na serikali ya Beijing.