Iraq yatangaza kuudhibiti mji wa Tikrit
Serikali ya Iraq imetangaza kwamba jeshi lake limefaulu kurejesha kwenye himaya yake mji wa Tikrit, ambao ulikua bado mikononi mwa kundi la wanamgambo wa Dola la Kiislamu. Taarifa hii imethibitishwa Jumanne wiki hii na waziri mkuu wa Iraq, Haïdar al-Abadi.
Imechapishwa:
Hata hivyo ni vigumu kuthibitisha taarifa hii, lakini inaaminika kwamba majeshi ya Iraq yamefaulu kuyadhibiti baadhi ya maeneo yaliyokua yakishikiliwa na kundi la wapiganaji wa Dola la Kiislamu.
Baada ya kuteka majengo kadhaa ya serikali katika mkoa wa Tikrit na hospitali kuu ya mjii mkoa huo, ni dhahiri kwamba majeshi ya Iraq yameendelea kufanya vizuri dhidi ya kundi hili la wanamgambo wa kiislamu tangu mapigano yalipoanza katika mkoa huo wa Tikrit, mwezi mmoja uliyopita. Waziri mkuu wa Iraq Haïdar al-Abadi, ameseama kuwa wamepata ushindi na kutangaza kwamba bendera zimerudi kupeperushwa kwenye majengo muhimu ya serikali katika mji huo.
Hata hivyo mapigano bado yanaendelea. Kwa mujibu wa msemaji wa muungano unaoongozwa na Marekani dhidi ya kundi la wapiganaji wa Dola la Kiislamu, baadhi ya maeneo ya mji yameendelea kushikiliwa na wapiganaji wa kiislamu.
Wapigaanaji wa kundi la Dola la Kiislamu bado wana uwezo wa kukabiliana na majeshi ya muungano. Hata hivyo kuna vilipuzi na mabomu mengine ambayo yametegwa kwenye baadhi ya mitaa ya mji wa Tikrit.
Pengine itachukua wiki kadhaa kwa vikosi vya serikali ili kutegua mabomu hayo yaliyotegwa na wapiganaji wa kiislamu.