Wakazi wa Bangkok wameanza kuyahama makazi yao wakati Serikali ikitoa siku 5 za mapumziko
Wananchi wa Thailand wameanza kuyahama makazi yao katika Mji Mkuu Bangkok wakikimbia mafuriko ambayo yanaukumba Mji huo kwa lengo la kukimbia hatarai ya kuchukuliwa na maji ambayo yamechangiwa na mvua iliyoshuhudiwa kwa majuma matatu sasa.
Imechapishwa:
Serikali nchini Thailand imetangaza siku tano za mapumziko kwa wananchi wa taifa hilo ili waweze kutumia muda huo kukabiliana na madhara ambayo yanaweza kuchangiwa na mafuriko ambayo yameshafika kati kati ya Bangkok.
Mapumziko hayo ya siku tano ambayo yametangazwa na serikali yametoa fursa kwa wananchi wa Bangkok kuanza kusaka maeneo ambayo ni salama wakikimbia maji ambayo yamezagaa kwenye sehemu kubwa ya Mji huo.
Wananchi wamelazimika kukimbia madhara zaidi ya mafuriko hayo kwani hadi sasa juhudi ambazo zimechukuliwa na serikali ya Waziri Mkuu Yingluck Shinawatra zinaonekana kutozaa matunda ambayo yalikuwa yanatarajiwa.
Tayari serikali ya Thailand iliamua kudhibiti maji hayo kwa kutumia vifuko vya mchanga ambavyo vilisambaza maeneo mbalimbali ya taifa hili lakini hata hivyo njia hiyo imeonekana kugonga mwamba kwa sasa.
Uamuzi wa serikali kutoa mapumziko ya siku tano ulionekana kupingwa vikali na Taasisi za Kibenki ikiwemo Benki Kuu ya Thailand ambapo wenyewe waliamua kuendelea kufanyakazi kwa kuhofia kutetereka kwa uchumi.
Takwimu rasmi ambazo zimetolewa na serikali ya Thailand zinaonesha kuwa watu zaidi ya mia tatu wamepoteza maisha tangu kuanza kwa mafuriko yaliyochangiwa na mvua za masika zilizoanza mwezi Julai.