Mahakama ya Bolivia yatoa waranti dhidi ya Evo Morales
Baada ya majuma kadhaa ya machafuko ya baada ya uchaguzi nchini Bolivia, ambayo yalisababisha kujiuzulu kwa Evo Morales, anayetuhumiwa kwa udanganyifu wa uchaguzi, rais huyo wa zamani wa Bolivia anasakwa na mahakama nchini humo.
Imechapishwa:
Waranti wa kukamatwa ulitolewa Desemba 18 na majaji wawili wanaopambana na ufisadi.
Kwa mujibu wa mwandishi wetu La paz ,Alice Campaignolle, Bw Morales anashtumiwa makosa matatu ikiwa ni pamoja na kusababisha machafuko, ugaidi na kufadhili ugaidi.
Morales alichukua uamuzi wa kujiuzulu katika kile kinachoonekana kuwa ni mapinduzi baridi na shinikizo kutoka kwa jeshi.
Evo Morales alimshinda mpinzani wake Carlos Mesa katika uchaguzi wa urais uliofanyika hivi karibuni nchini humo. Pamoja na ushindi wake huo, wapinzani nchini Bolivia wamepinga matokeo hayo ya uchaguzi wa urais.
Evo Morales alinukuliwa akisema: Mahasimu wa kisiasa wanajiandaa kufanya mapinduzi na mrengo wa kulia umeandaa mapinduzi kwa msaada wa kimataifa. 'Ninalaani mapinduzi ambayo yamo mbioni kutokea, mapinduzi ambayo yamo katika hali ya kutokea kwa himaya na uungaji mkono wa kimataifa'.
Bw Morales aliondoka nchini Bolivia kwenda uhamishoni nchini Mexico, baada ya kupata hifadhi ya kisiasa.